Wantam: Sifuna aoshewa lami, apokelewa kishujaa Bungoma
KIFO cha aliyekuwa Waziri Mkuu Raila Odinga kimebadilisha kwa kiasi kikubwa mwelekeo wa siasa za Kenya, huku Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna akiibuka kama mmoja wa viongozi wanaotikisa hesabu za uchaguzi mkuu wa 2027.
Baada ya kuondolewa kama Katibu Mkuu na msemaji wa ODM, Sifuna sasa anaongoza vuguvugu la Linda Mwananchi, ambalo wachambuzi wanasema linaweza kubadili kabisa sura ya siasa za nchi na kutatiza mipango ya serikali pamoja na upinzani.
Ndani ya ODM, baadhi ya viongozi wanakiri kuwa kumuondoa Sifuna kutoka uongozi wa chama kulikuwa kosa kubwa. Hata hivyo, sasa anaongoza vuguvugu linalovutia wafuasi wengi, hasa vijana, na ambazo zinazidi kupata nguvu kote nchini.
Umaarufu wake umewatia wasiwasi viongozi wa kisiasa wa Magharibi kama Spika wa Bunge la Kitaifa Moses Wetang’ula na Mkuu wa Mawaziri Musalia Mudavadi, ambao wamekuwa wakijitambulisha kama vinara wa eneo hilo.
Jana, Sifuna aliongoza mikutano mikubwa ya kisiasa katika Kaunti ya Trans Nzoia na kutangaza kuwa yuko tayari kuwania urais katika uchaguzi mkuu wa 2027.
Akizungumza katika mkutano wa mwisho mjini Kitale, Sifuna alimshukuru Gavana wa Trans Nzoia George Natembeya kwa kumuunga mkono na kumhimiza azunguke nchi nzima kutafuta uungwaji mkono.
“Nimekubali jukumu hilo. Niko tayari kuzunguka Kenya nzima kutafuta kura na sitawaangusha Wakenya,” alisema.
Sifuna alidai kuwa upinzani utaungana na kumteua mgombeaji mmoja wa urais atakayemenyana na Rais William Ruto katika uchaguzi ujao.
Baada ya mikutano hiyo, msafara wa viongozi hao ulipitia Kaplamai na kusimama katika soko la Sibanga, Cherang’any, kabla ya kurejea Kitale kwa mkutano wa mwisho.
Kwa mujibu wa utafiti wa hivi karibuni wa TIFA uliotolewa Ijumaa, Sifuna amempiku kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka katika umaarufu wa urais kwa mara ya kwanza.
Katika utafiti huo, Sifuna alipata asilimia 15 ya uungwaji mkono, akifuatiwa na Naibu Kiongozi wa Jubilee Fred Matiang’i kwa asilimia 14, Kalonzo Musyoka asilimia 13, kiongozi wa DCP Rigathi Gachagua asilimia saba na Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino asilimia mbili.
Kwa jumla, viongozi wa upinzani wanaungwa mkono na asilimia 51 ya Wakenya, huku Rais William Ruto akiongoza kivyake kwa asilimia 24. Hata hivyo, kiwango hicho bado hakitoshi kumwezesha kushinda uchaguzi katika duru ya kwanza.
Kinachowashangaza wengi si tu umaarufu wa Sifuna bali kasi aliyopanda nayo. Miezi miwili iliyopita hakuwa hata akitajwa katika mazungumzo ya wagombeaji urais. Sasa ameibuka kama mmoja wa wanasiasa wenye ushawishi mkubwa zaidi nchini.
Katika uchaguzi wa Seneti wa Nairobi mwaka 2022, Sifuna alimshinda Askofu Margaret Wanjiru kwa kura 716,876. Leo, umaarufu wake unatajwa kuwa unaweza kubadili mazungumzo ya muungano wa upinzani kuhusu mgombeaji mmoja wa urais.
Hata baada ya kuondolewa katika uongozi wa ODM, utafiti unaonyesha karibu nusu ya wafuasi wa chama hicho wangependa awe mgombeaji wao wa urais.
Matokeo hayo yanaendana na utafiti wa awali wa Infotrak uliomuonyesha Sifuna akipunguza pengo kati yake na viongozi waliokuwa wakitajwa kama vigogo wa upinzani, jambo linaloashiria kuwa kupanda kwake si bahati bali ni mwelekeo mpya wa kisiasa.
Akizungumza baada ya matokeo ya utafiti huo kutolewa, Sifuna alisema jambo muhimu si asilimia aliyopata, bali ni kwamba Rais Ruto anaendelea kushuka chini ya kiwango kinachohitajika kushinda uchaguzi kwa urahisi.
Alisema iwapo upinzani utaungana nyuma ya mgombeaji mmoja, utaweza kumshinda Rais Ruto.
“Tukijumlisha asilimia za Sifuna, Kalonzo, Matiang’i na viongozi wengine wa upinzani, ziko juu zaidi ya za Rais Ruto. Tunahitaji umoja ili kuwasikiliza Wakenya wanaotaka mabadiliko,” alisema.
Mchambuzi wa siasa Arnold Maliba alisema wengi wanakosea kuchukulia Linda Mwananchi kama muungano wa kawaida wa kisiasa.
Kwa mujibu wake, vuguvugu hilo linalenga kubadili mjadala wa kisiasa kutoka ukabila na makubaliano ya viongozi kuelekea masuala ya utawala bora, uwajibikaji, Katiba na ushiriki wa wananchi.
“Linda Mwananchi si chama cha kawaida. Ni vuguvugu linaloweka shinikizo kwa serikali na pia kwa upinzani uliopo,” alisema.
Kwa Rais Ruto, kupanda kwa Sifuna kunamaanisha hatari ya kupoteza kura za eneo la Magharibi, ambazo ni muhimu katika azma yake ya kutetea urais, hasa baada ya kupoteza uungwaji mkono mkubwa katika Mlima Kenya.
Ndani ya upinzani, kuibuka kwa Sifuna kumebadili hesabu zilizoweka Kalonzo Musyoka na Fred Matiang’i kama wagombeaji wakuu wa urais.