Gharama ya kusafirisha mizigo kupanda baada ya kuongezeka kwa bei ya mafuta
GHARAMA ya kusafirisha bidhaa nchini na katika ukanda mzima imeongezeka kwa asilimia 14 kuanzia leo, kufuatia tangazo la Jumanne jioni la Mamlaka ya Kudhibiti wa Kawi na Petroli (EPRA) la kuongeza bei ya mafuta kwa Sh40 kwa lita kutoka Sh163.
Tangazo hilo la EPRA lilifichua kuwa bei ya mafuta imeongezeka kwa asilimia 24.5 kwa jumla.
Athari ya ongezeko hilo imeanza kuhisiwa kwenye bidhaa zinazosafirishwa kutoka Bandari ya Mombasa na pia katika sekta ya viwanda, hali hiyo ikitarajia itachangia ongezeko la bei sokoni.
Mwenyekiti wa Chama cha Wasafirishaji wa Mizigo Kenya (KTA), Newton Wang’oo, kwenye taarifa kwa wanachama wake, aliwataka wawasiliane na wateja wao pamoja na washirika wa kibiashara kuwaeleza wazi sababu za kuongeza bei.
KTA, inasimamia zaidi ya malori 6,000 yanayosafirisha bidhaa kutoka Bandari ya Mombasa na kote nchini. Chama hicho kilisema wanachama wake hawawezi kubeba gharama kubwa inayotokana na kupanda kwa bei ya mafuta, hivyo italazimu mzigo huo uhamishiwa kwa watumiaji wa bidhaa hiyo.
Bw Wang’oo alisema mafuta ndiyo sehemu kubwa zaidi ya gharama katika uchukuzi wa barabarani, yakichangia asilimia 55 ya gharama zote za kuendesha biashara hiyo.
“Wanachama wanakumbushwa kuwa mafuta ndiyo gharama kuu katika usafirishaji wa mizigo kupitia barabara, yakichangia karibu asilimia 55 ya gharama zote za kibiashara. Hii inafasiriwa kuwa ongezeko la asilimia 13 hadi 14 ya gharama za usafirishaji kwa ujumla,” akasema Bw Wang’oo.
Aliongeza kuwa ongezeko hilo kubwa la gharama haliwezi kuhimiliwa na wanachama, ndiposa gharama yao ikiongezeka, bei mpya pia inastahili kuwekwa.
Ingawa hivyo, KTA kujitolea kulinda maslahi ya wanaosafirisha bidhaa nchini na eneo zima la Afrika Mashariki.
Kuongeza bei ya dizeli na petroli kwa kati ya Sh28 hadi Sh40 kwa lita kunatarajiwa kuongeza nauli za usafiri wa umma pamoja na gharama za usafirishaji wa mizigo.
Hali hii itaathiri moja kwa moja bei ya vyakula kutokana na gharama kubwa za uzalishaji na usafirishaji.