Wamiliki wa malori wapandisha gharama za usafirishaji kufuatia kupanda kwa bei ya mafuta
Chama cha Wamiliki wa Malori nchini, (TAK), kimeagiza wanachama wake kuongeza gharama za usafirishaji kwa asilimia 30, kikitaja kupanda kwa bei ya mafuta kufuatia ongezeko la hivi punde la bei lililotangazwa na Mamlaka ya Kudhibiti Kawi na Petroli (EPRA).
Chama hicho, kinachowakilisha wanachama 20,000 waliosajiliwa na zaidi ya malori 50,000, kilisema viwango hivyo vipya vinaanza kutekelezwa mara moja.
Wakizungumza na wanahabari mjini Syokimau, Kaunti ya Machakos, Jumatano, maafisa wa TAK pia walielezea wasiwasi wao kuhusu uhaba wa mafuta ulioshuhudiwa hivi karibuni, wakijiuliza kwa nini bidhaa za petroli sasa zinapatikana kwa wingi katika vituo ambavyo hapo awali vilidai vilikuwa vimedai vimekaukiwa.
Walidai huenda kulikuwa na udanganyifu wa makusudi katika usambazaji wa mafuta.
Kulingana na mwenyekiti wa chama hicho, Raphael Lamuya, serikali ilikuwa imewahakikishia Wakenya kuwa nchi ina akiba ya kutosha ya mafuta, lakini baadaye ikapandisha bei — hatua aliyosema inaonyesha ukosefu wa mipango na mawasiliano duni.
“Tulihakikishiwa kuwa nchi ina akiba ya kutosha ya mafuta lakini tunachoshuhudia sasa ni kupanda kwa ghafla kwa bei. Ongezeko hili litawaumiza moja kwa moja wasafirishaji ambao watalazimika kuwahamishia gharama hizi kwa walaji, na hivyo kuathiri uchumi kwa jumla. Hali hii inazua maswali makubwa kuhusu namna usambazaji na bei ya mafuta unavyosimamiwa. Tayari tumewaagiza wanachama wetu wote kuongeza gharama za usafirishaji hadi asilimia 30. Kuna uwezekano biashara kupungua kutokana na gharama ya juu, lakini kama wasafirishaji hatuna budi ila kuongeza bei,” alisema Lamuya.
Katibu Mkuu wa chama hicho, Denny Kilia, alihimiza serikali kuchukua hatua za tahadhari, ikiwemo kuhakikisha kuna akiba ya mafuta inayoweza kudumu kwa hadi mwaka mmoja ili kulinda nchi dhidi ya misukosuko ya baadaye.
“Serikali lazima iweke mikakati ya muda mrefu ya kudhibiti usambazaji wa mafuta. Hatuwezi kuendelea kufanya kazi katika hali ya sintofahamu kila baada ya miezi michache. Kuwa na akiba ya kimkakati ya angalau mwaka mmoja kutalinda nchi dhidi ya mishtuko kama hii,” aliongeza.
Kwa mujibu wa bei mpya, dizeli — ambayo ndiyo hutumiwa na malori — sasa inauzwa kwa Sh206 kwa lita, ikiwa ni ongezeko la Sh40. Petroli pia sasa inauzwa kwa Sh206 kwa lita, ikiwa imeongezeka kwa Sh28.
Madereva wa malori wameonya kuwa kupanda kwa gharama za usafirishaji kutasababisha athari kwa uchumi mzima, hali ambayo inaweza kuongeza bei ya bidhaa na huduma.
“Ongezeko la asilimia 30 la gharama za usafirishaji hatimaye litahamishiwa kwa watumiaji. Hii inamaanisha bei ya bidhaa za msingi itapanda, na mwishowe ni Mkenya wa kawaida atakayebeba mzigo huo,” aliongeza Kilia.