Kaunti ya Wantam? Ushindani mkali wengi wakijitokeza kuwania ugavana Taita Taveta
USHINDANI mkali wanukia katika Kaunti ya Taita Taveta huku idadi ya wanaotaka kuwania ugavana ikiongezeka.
Gavana wa kaunti hiyo, Bw Andrew Mwadime, na naibu wake Bi Christine Kilalo wanaendelea kuwahimiza wakazi kuwaongezea muhula wa pili ili kukamilisha miradi yao ya maendeleo.
Taita Taveta haijawahi kuwa na gavana aliyehudumu kwa mihula miwili.
Gavana wa kwanza, Bw John Mruttu, alishindwa 2017 na Bw Granton Samboja, ambaye naye alishindwa na Bw Mwadime 2022.
Hata hivyo, Bw Samboja anapanga kuwania tena wadhifa huo mwaka ujao.
Wengine waliojitokeza ni Mbunge wa Wundanyi Danson Mwashako (Wiper), Seneta Jones Mwaruma (ODM), Katibu wa Leba Shadrack Mwadime, Meneja wa Uhandisi katika Bandari ya Mombasa Anderson Mtalaki, na aliyekuwa Kaimu Mkurugenzi wa KPA John Mwangemi.
Bw Mruttu (UDA) sasa amehamia kinyang’anyiro cha useneta huku Bw Mwadime, aliyeshinda ugavana akiwa mgombea huru, akiashiria nia ya kutetea kiti chake kupitia UDA.