Habari za Kaunti

Mgomo wa mafuta waanika jinsi Mombasa hutegemea bara kwa chakula

Na BRIAN OCHARO May 21st, 2026 Kusoma ni dakika: 2

UPUNGUFU mkubwa wa bidhaa muhimu katika Soko la Kongowea mjini Mombasa wakati wa mgomo kuhusu bei ya mafuta uliotamatika Jumanne, ulifichua jinsi jiji hilo hutegemea kikamilifu usambazaji wa chakula kutoka nje ya kaunti.

Kila siku, malori kutoka maeneo ya bara husafirisha mazao ya kilimo hadi sokoni, ambako wakazi hununua chakula kwa matumizi ya nyumbani huku wauzaji wadogo wakinunua bidhaa kutoka kwa wauzaji wa jumla.

Mgomo ulianza Jumatatu hadi Jumanne uliwaacha wafanyabiashara sokoni wakikadiria hasara, na wakazi kulazimika kununua bidhaa chache kwa bei ya juu.

Wasafirishaji bidhaa hawakuelekea Mombasa kwa hofu kwamba malori yao yangevamiwa au kuteketezwa barabarani.

Bw Peter Mutisya, mwenyekiti wa sehemu ya uuzaji ndizi sokoni, alisema eneo hilo linategemea sana usambazaji kutoka Meru na Taveta, lakini mizigo haikuwasili.

“Kawaida tunapokea kati ya malori sita hadi saba ya ndizi kila siku, lakini kwa siku mbili zilizopita hakuna mzigo wowote uliwasili kwetu kwa sababu wasafirishaji walikuwa na hofu magari yao yatateketezwa,” alisema.

Ingawa mgomo ulisitishwa, vyama vya watumiaji wa mafuta vilisema wanachama wao watagoma tena ikiwa hakutakuwa na makubaliano na serikali ndani ya wiki moja.

Bw Mutisya alionya kuwa ikiwa hali hiyo itaendelea, soko linaweza kukumbwa na upungufu mkubwa wa bidhaa, akibainisha kuwa wafanyabiashara wengi wanaotegemea mikopo kuendesha biashara zao walipata shida kutokana na kupungua kwa mauzo.

“Tunaomba serikali na wadau wote kushiriki mazungumzo na kutatua mgogoro huu kabla biashara hazijaporomoka,” alisema.

Katibu Mkuu wa Soko la Kongowea Veronica Wachira, alisema idadi ya magari yanayoleta mboga sokoni ilipungua kwa kiasi kikubwa na kuwaacha wafanyabiashara wakiteseka.

“Siku ya kawaida tunapokea hadi malori 10 yanayobeba sukuma wiki, mchicha na mboga nyingine, lakini leo gari moja pekee ndilo limewasili. Ikiwa hali hii itaendelea, hatutakuwa na chakula sokoni,” alisema.

Bi Wachira alieleza kuwa, mboga nyingi zinazouzwa sokoni huharibika haraka na zinahitaji usambazaji wa kila siku, lakini wasafirishaji walikuwa wakisita kusafiri kutokana na hofu ya kushambuliwa barabarani.

Naibu mwenyekiti wa sehemu ya viazi, Bw Caleb Ndirangu, alisema usambazaji wa bidhaa hiyo pia uliathirika sana, hali iliyosababisha kupanda kwa bei na kuwaacha wafanyakazi wa vibarua bila kazi.

“Kawaida karibu malori 30 ya viazi huwasili kila siku, lakini katika siku mbili zilizopita ni malori manne pekee yaliingia,” alisema.

Bw Ndirangu aliongeza kuwa, bei ya gunia la kilo 95 la viazi ilipanda kutoka karibu Sh4,500 hadi Sh8,000 kutokana na upungufu huo, jambo lililofanya bidhaa hiyo kuwa ghali kwa wateja.

Pia alibainisha kuwa, gharama za usafirishaji kutoka maeneo yanayozalisha viazi kama Molo, Nakuru na Nyandarua zimeongezeka kwa kiasi kikubwa kutokana na kupanda kwa bei ya mafuta.

“Awali tulikuwa tunalipa karibu Sh60,000 kusafirisha lori la viazi hadi Mombasa, lakini sasa gharama imepanda hadi karibu Sh90,000. Ikiwa hali itaendelea hivi, wafanyabiashara wengi wanaweza kulazimika kufunga biashara zao,” alisema.