Habari za Kaunti

Wakazi waeleza kutoridhishwa na mkutano wa kutolea maoni Mswada wa Fedha

Na KEVIN MUTAI June 10th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WAKAZI wa Mombasa wameelezea kutoridhishwa na jinsi mkutano wa kushirikisha umma kuhusu Mswada wa Fedha wa 2026 ulivyofanyika.

Huku wakikosoa hatua za ushuru zilizopendekezwa, walitilia shaka kujitolea kwa Bunge kusikiliza maoni yao.

Baadhi ya washiriki walilalamika kuwa mapendekezo hayo hayakuelezwa kwa kina, huku wengine wakiwashutumu viongozi kwa kutumia ushirikishwaji wa umma kama utaratibu wa kutimiza matakwa ya Katiba bila nia ya kusikiliza maoni yao.

Wakazi kadhaa pia walitaka Bunge kudhibiti kile walichokitaja kuwa matumizi ya kifahari ya fedha za umma na safari za mara kwa mara za nje ya nchi badala ya kulenga kutoza ushuru zaidi kuongeza mapato.

Kikao hicho kilifanyika katika Ukumbi wa Tononoka na kiliandaliwa na Kamati ya Bunge ya Fedha na Mipango ya Kitaifa mnamo Jumatatu.

Kikiongozwa na mwenyekiti wa kamati hiyo na Mbunge wa Molo Kimani Kuria, kikao hicho kilihudhuriwa na wakazi kutoka kaunti ndogo zote sita za Mombasa.

Kwa mujibu wa Simon Aloo, mkazi wa Kadzandani katika Kaunti Ndogo ya Nyali, mchakato huo ulipaswa kuwapa Wakenya na wadau wengine nafasi ya kuchambua kwa kina mapendekezo ya ushuru, lakini washiriki wengi hawakuwa na taarifa za kutosha kuelewa mapendekezo hayo.

Akijibu, Bw Kuria alisema kuwa mswada huo una zaidi ya viambatisho 10 vinavyopendekeza nafuu mbalimbali za ushuru kwa Wakenya.

“Wafanyabiashara wanataka ushuru mmoja tu utozwe kwa mitumba inapoingia nchini na waepushwe na tozo nyingine kama ushuru wa kampuni wa asilimia 30 unaotozwa faida halisi,” akaeleza.

Kwa mujibu wa Omar Jilo kutoka Kaunti Ndogo ya Kisauni, Bunge limewaangusha Wakenya katika jukumu lake la usimamizi na linafaa kutumia mamlaka yake ya usimamizi kuweka mifumo madhubuti ya kudhibiti bajeti ya safari za viongozi.

“Kama Bunge ni wawakilishi wetu, kwa nini wasidhibiti safari za rais nje ya nchi na kuhakikisha fedha zinazotumika zinapunguzwa?” alihoji.

Wengine walihoji uhalali wa mikutano hiyo ya ushirikishwaji wa umma wakisema kuwa wananchi hawakuelimishwa vya kutosha kuhusu miswada hiyo na hawakupewa nafasi ya kutosha ya mjadala.

Pia waliikosoa kamati hiyo kwa kushindwa kujibu ipasavyo kile walichokiita mapendekezo muhimu ya mapato yanayolenga walipa kodi.

“Je, ni haki kufanya hamasisho ya umma kuhusu Mswada wa Fedha wa 2026 kwa saa moja pekee? Haya ni maisha yetu na nafikiri muda huo hautoshi,” alisema Bw Ali Hassan.