Habari za Kitaifa

Chebukati alisimamia uchaguzi wa urais wa kwanza kubatilishwa Kenya

Na SAMWEL OWINO February 21st, 2025 Kusoma ni dakika: 2

WAFULA Wanyonyi Chebukati, aliyesimamia uchaguzi wa urais uliobatilishwa na Mahakama mwaka wa 2017 na wa 2022 uliogawanya Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) amefariki dunia akiwa na umri wa miaka 63.

Bw Chebukati alikamilisha kipindi chake cha miaka sita akiwa mwenyekiti wa IEBC mnamo Januari 17, 2023.

Muhula wake kama Mwenyekiti wa IEBC ulianza Januari 2017 kufuatia kuondolewa kwa Ahmed Issack Hassan na makamishna wenzake.

Wakili huyo alichukua wadhifa huo wakati uliojaa joto la kisiasa, huku kiongozi wa upinzani Raila Odinga akikabiliana na Rais Uhuru Kenyatta, ambaye alikuwa akigombea kwa muhula wa pili.

Bw Chebukati na timu yake walitwikwa jukumu la kufanya mojawapo ya uchaguzi uliokuwa na ushindani mkubwa nchini Kenya ambao waliandaa kwa muda wa chini ya miezi saba.

Hata hivyo, uchaguzi wake wa kwanza kusimamia ulipingwa na matokeo ya kura za urais mwaka wa 2017 yakabatilishwa na Mahakama ya Juu katika uamuzi wa kihistoria.

Katika uamuzi wake, mahakama ya upeo, wakati huo ikiongozwa na Jaji Mkuu David Maraga, iligundua kuwa uchaguzi alioshinda Uhuru Kenyatta dhidi ya Raila Odinga ulikumbwa na dosari na ukiukaji wa sheria huku ikilaumu IEBC.

Mahakama ya Juu iliamuru uchaguzi mpya wa urais ufanyike ndani ya siku 60.

Hata hivyo, kiongozi wa upinzani Raila Odinga alisusia uchaguzi wa marudio, akisema kwamba hangeweza kushiriki uchaguzi uliosimamiwa na timu ile ile “iliyovuruga” ule wa awali.

Mara kwa mara, Bw Chebukati alizozana na mirengo ya kisiasa lakini alipinga wito wa kujiuzulu.

Uchaguzi wa urais wa 2022 haukuwa tofauti, kwani upinzani ulidai mgombeaji wao, Bw Odinga, alitapeliwa na kumpendelea William Ruto.

Upinzani, ambao ulipinga matokeo ya kura katika Mahakama ya Juu bila kufaulu, ulidai kuwa mfumo wa tume hiyo uliruhusu baadhi ya watu kuhujumu matokeo ya mwisho ili kumpendelea Dkt Ruto.

Hata hivyo, Mahakama ya Juu ilitupilia mbali madai hayo na kuidhinisha ushindi wa Dkt Ruto, ikitaja baadhi ya madai katika kesi kuwa ‘hewa’.

Katika maandalizi ya uchaguzi wa Agosti 2022, na wakati wa kujumlisha kura, mzozo mkali wa ndani uliibuka ndani ya tume, na kusababisha mgawanyiko kati ya makamishna.

Makamishna saba waligawanyika katika makundi mawili: moja likiongozwa na Bw Chebukati, Boya Molu, na Abdi Guliye, na lingine likiwa na naibu mwenyekiti Juliana Cherera, Francis Wanderi, Irene Masit na Justus Nyang’aya.

Vita baridi ndani ya IEBC viliendelea, lakini vililipuka  hatimaye makamishna wanne walipopinga hadharani kuwasilishwa kwa matokeo ya uchaguzi wa urais.

Makamishna Francis Wanderi, Irene Masit, Justus Nyang’aya na Makamu Mwenyekiti Juliana Cherera walipinga baadhi ya matokeo yaliyotangazwa na Bw Chebukati wakidai hayakuwa yamethibitishwa na makamishna wote.

Makamishna waliojitenga waliondoka Bomas ya Kenya na kufanya mkutano na waandishi wa habari katika Hoteli ya Serena, ambapo walikataa matokeo ya urais yaliyotangazwa na tume.

Walimkashifu Bw Chebukati kwa kupuuza mapendekezo yao wakisema kuwa alijiteua kuwa afisa wa kitaifa wa uchaguzi wa urais. Mwenyekiti huyo alishinda kwa kuwa baada ya mvutano,  makamishna waliompinga, ambao walifahamika kama Cherera Four, waliondoka kwenye tume hiyo huku mmoja wao, Bi Masit, akitimuliwa baada ya jopo la mahakama kubuniwa kuchunguza mwenendo wake.

Ingawa baadhi walimwona Bw Chebukati kama kiongozi aliyekuwa na kichwa ngumu, wengine walimwona kama mtu thabiti, asiyeyumbishwa na nguvu za nje.

Baada ya kuondoka madarakani mwishoni mwa muhula wake wa miaka sita, Bw Chebukati hakuonekana hadharani, huku ripoti zikisema kuwa afya yake ilikuwa ikidorora.

Bw Chebukati aliyezaliwa Desemba 19, 1961, alikuwa na Shahada ya Kwanza ya Sheria kutoka Chuo Kikuu cha Nairobi, na Uzamili katika Utawala wa Biashara kutoka Chuo Kikuu cha Kilimo na Teknolojia cha Jomo Kenyatta.

Alikuwa mwanasiasa na mwanachama wa chama cha Orange Democratic Movement lakini alijiuzulu kabla ya kutuma maombi ya kuwa Mwenyekiti wa IEBC. Mnamo 2007, aligombea kiti cha eneobunge la Saboti na kuibuka wa pili.