Habari za Kitaifa

Anayeshukiwa kuua mpenziwe majuu na kurejea Kenya asubiri kusafirishwa London kujibu kesi

Na RICHARD MUNGUTI June 15th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MKENYA aliyekuwa anaishi na kufanya kazi Uingereza amezuiliwa rumande akisubiri kurudishwa London kujibu mashtaka ya kumuua mpenziwe Maryanne Nduta Januari 2025.

Mahakama ya Milimani Nairobi wiki jana iliamuru Brian Kiprop Kipglagat aliyetorokea nchini baada ya kutekeleza uhalifu huo asalie ndani hadi mustakabali wa kumrudisha ulaya kujibu mashtaka utakapokamilishwa kati ya Serikali za Kenya na Uingereza.

Kiplagat alikamatwa Juni 10, 2026 katika mpaka wa Kenya na Tanzania.

Sasa, Kiplagat anazuiliwa chini ya ulinzi mkali katika kitengo cha polisi wa kupambana na ugaidi (ATPU).

Alifikishwa mbele ya Hakimu Mwandamizi mahakama ya Milimani Daisy Mutai Juni 12, 2026 baada ya kuzuiliwa katika kituo cha mpakani cha Namanga.

Mahakama ilielezwa na mkurugenzi wa mashtaka ya umma kwamba Kiplagat anatarajiwa kushtakiwa kwa mauaji ya Maryanne, aliyekuwa mfanyakazi wa Benki ya London.

“Baada ya kutekeleza mauaji hayo, Kiplagat alitorokea Kenya. Makachero wamekuwa wakimsaka kwa udi na uvumba,” kiongozi wa mashtaka Bi Joyce Olajo alieleza mahakama.

Kitengo cha Polisi cha Metropolitan cha Uingereza kilipata kibali cha kumtia nguvuni Kiplagat. Hakikufanikiwa. Alikuwa ametorokea Kenya.

Maafisa hao wa polisi wa Ulaya waliomba polisi wa kimataifa (Interpol) jijini Nairobi kusaidiana na Huduma ya Kitaifa ya Polisi (NPS) kumsaka na kumkamata mshukiwa huyu kurejeshwa London kujibu mashtaka ya mauaji.

“Serikali ya Kenya kupitia Wizara ya Mashauri ya Kigeni ilipokea ombi kutoka Uingereza Kiplagat akamatwe na kurudishwa nchini humo kushtakiwa kwa mauaji ya Maryanne Nduta,” Bi Olajo alimweleza hakimu.

Mahakama ilifahamishwa mshukiwa huyo aliomba kibali cha kuingia Tanzania mnamo Juni 10, 2026 kisha akaanza safari ya kutoroka.

Katika kituo cha mpakani cha Namanga, Bw Kiplagat alitambuliwa ndipo akatiwa nguvuni.

Alifikishwa mahakamani kisha korti ikaombwa imzuilie kwa siku 21 kuwezesha serikali kukamilisha utaratibu wa kumkabidhi kwa maafisa wa polisi wa Interpol arudishwe Uingereza kushtakiwa kwa mauaji ya Maryanne Nduta.

Mahakama ilielezwa kwamba Kenya na Uingereza ziko na mkataba wa kubadilishana washukiwa wa uhalifu.

“Mshtakiwa atafunguliwa shtaka la kuua kinyume cha sheria nambari 203 na 304 za sheria za jinai za Uingereza. Sheria hii ni sawa na sheria za Kenya kwa kuwa nchi hii ilirithi sheria zote kutoka kwa walowezi,” Bi Olajo akaeleza korti.

Mahakama iliamuru mshukiwa huyo asalie korokoroni hadi Juni 15, 2026 kwa maagizo zaidi.

Kiplagat aliamriwa azuiliwe katika idara ya ATPU hadi ombi la serikali la kumsafirisha hadi Uingereza lisikizwe na kuamuliwa.