Majambazi waliohepa na majeraha ya risasi wasakwa
POLISI katika Kaunti ya Mombasa wanaendelea kuwasaka wahalifu waliotoroka na majeraha ya risasi, baada ya mpango wao wa kuiba gari katikati ya jiji kutibuliwa.
Katika tukio lililotokea Jumatano iliyopita, majambazi watatu walikabiliana kwa risasi na polisi katika Barabara ya Kenyatta, ambako walipatikana wakivunja na kuiba mali kutoka kwenye gari lililokuwa limeegeshwa huku mmiliki wake akiwa ndani ya mkahawa wa karibu.
Walitoroka kutoka eneo la tukio kwa kutumia gari lao kabla ya kuliacha barabarani walipokuwa wakifuatwa na polisi hadi eneo la King’orani.
Kamanda wa Polisi wa Kaunti Ndogo ya Mvita Nicholas Chalulot, alisema maafisa wa upelelezi walikuwa wameitikia simu ya dharura kutoka kwa mmiliki wa gari hilo baada ya kugundua kuwa mali zake zilikuwa zikiibwa alipokuwa akila katika mkahawa wa karibu.
“Walifyatua risasi mbili na maafisa wetu walipojibu, waliondoka kwa kasi. Msako ukaanza na walipogundua kuwa walikuwa wamezingirwa, waliliacha gari lao na kutoroka kwa miguu kuelekea eneo la King’orani,” alisema Bw Chalulot.
Wapelelezi wanasema tukio hilo limefichua mtindo mpana wa wizi unaolenga magari yaliyoegeshwa katika maeneo yote Mombasa.
Polisi wanaamini kundi hilo limekuwa likivamia magari yaliyoegeshwa hasa nyakati za usiku na kutumia magari ya wizi waliyowekea nambari bandia za usajili kutoroka.