Habari za Kitaifa

Kalonzo aruhusiwa kuona Gachagua hospitalini, akosoa seneti

Na DANIEL OGETTA, BENSON MATHEKA October 18th, 2024 Kusoma ni dakika: 1

KIONGOZI wa Wiper Kalonzo Musyoka amesema ameruhusiwa kumuona Naibu Rais aliyetimuliwa mamlakani Rigathi Gachagua katika hospitali ya Karen.

Akizungumza muda mfupi baada ya kukutana na kiongozi huyo aliyetimuliwa, Bw Musyoka alisema Gachagua anaendelea kupata nafuu.

Yeye, kiongozi wa chama cha DAP – Kenya Eugene Wamalwa na Seneta Joe Nyutu walikuwa wanasiasa wa kwanza kumuona Gachagua tangu Almisi usiku, Oktoba 17, 2024.

“Tuna bahati kwamba baadhi yetu tumeweza kuruhusiwa kumuona. Mimi mwenyewe, Wamalwa na Nyutu tumemwona,” Bw Musyoka alieleza.

Mungu kuokoa maisha yake

“Tunamtakia Gachagua afueni ya haraka sana. Tunamshukuru Mungu kwamba ameyaokoa maisha yake.”

Bw Gachagua aliugua hoja ya kumtimua ikisikilizwa katika Seneti jana usiku (Alhamis).

Alitarajiwa kujitetea mbele ya maseneta, afya yake ilipodhoofika.

Maseneta hao walimtimua alipokuwa hospitalini.

Lakini Bw Kalonzo alikosoa hatua hiyo, haswa baada ya Bw Gachagua kulazwa hospitalini.

“Sheria ya haki inadai kwamba hakuna mtu atakayehukumiwa bila kusikilizwa. Mawakili wa Gachagua watapinga hilo,” alisema Musyoka.

“Haki itawale katika mahakama zetu,” alisema.

Bw Wamalwa, kwa upande wake, alitaja Alhamisi usiku seneti ilipoidhinisha kuondolewa kwa Bw Gachagua, kama siku ya huzuni kwa nchi.

Kiongozi huyo wa DAP-K alimsifu Bw Gachagua kwa kuchagua “kuwakabili wanaomshtaki badala ya kusalimu amri.”

“Iwapo tulitilia shaka kuwa bunge limetekwa na serikali, jana usiku ulikuwa ushahidi,” Bw Wamalwa alisema.