Habari za Kitaifa

Mwanasheria Mkuu akosa kujibu iwapo waliotimuliwa afisini wanaweza kuwania 2027

Na JOSEPH WANGUI August 19th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MZOZO wa kisheria kuhusu iwapo viongozi waliotimuliwa afisini kupitia bunge wanaweza kugombea nyadhifa za kisiasa kabla ya kesi zao kukamilika bado utaendelea kushuhudiwa nchini.

Hii ni baada ya Mwanasheria Mkuu Dorcas Oduor, kukosa kutoa jibu la moja kwa moja kuhusu utata huo.

Suala hilo lina umuhimu mkubwa kwa aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua na aliyekuwa Gavana wa Meru Kawira Mwangaza, ambao wote waliondolewa mamlakani na Bunge na wanapinga kutimuliwa kwao kortini.

Bi Oduor ameishauri Mahakama ya Juu kutosikiza ombi la kutoa ushauri wa kikatiba kuhusu iwapo viongozi walioondolewa mamlakani kupitia bunge wanaweza kugombea nyadhifa za kisiasa kesi zao zikiendelea mahakamani.

Mawakili wa Spika wa Bunge la Kaunti ya Meru, Ayub Bundi, hata hivyo, wamesema Mwanasheria Mkuu hakujibu maswali manane ambayo Mahakama ya Juu ilimtaka kuyashughulikia.

Mawakili wa Spika wa Bunge la Kaunti ya Meru, Ayub Bundi, hata hivyo, walisema Mwanasheria Mkuu hakujibu maswali manane ambayo Mahakama ya Juu ilimtaka kuyajibu.

Mojawapo ya maswali hayo ni iwapo rufaa au kesi ya kupinga kuondolewa mamlakani inaweza kusimamisha amri ya kikatiba ya uamuzi huo na kumruhusu kiongozi huyo kugombea uchaguzi.

“Baada ya kupitia ushauri huo, ni wazi kwamba haujajibu wala kushughulikia masuala hayo,” wakasema mawakili hao.

Walimtaka Mwanasheria Mkuu kufuata maagizo ya Mahakama ya Juu kwa kutoa ushauri wa kisheria unaojibu kila swali lililowasilishwa.

Bw Gachagua aliondolewa mamlakani Oktoba 2024. Mahakama Kuu ilitupilia mbali kesi yake Juni 2026, lakini amekata rufaa katika Mahakama ya Rufaa.

Kiongozi huyo wa DCP ametangaza nia ya kuwania urais katika uchaguzi wa 2027.

Bi Mwangaza naye aliondolewa kama Gavana wa Meru Agosti 2024 baada ya Bunge la Kaunti kupitisha hoja ya kumtimua na Seneti kuithibitisha.

Mahakama Kuu ilikataa kesi yake Machi 2025, lakini amekata rufaa kupinga uamuzi huo.

Anaongoza chama cha Umoja na Maendeleo (UMP) na analenga kuwania kiti cha ugavana tena.

Bw Bundi aliwasilisha kesi hiyo katika Mahakama ya Juu Aprili 2026, akitaka ufafanuzi kuhusu masharti ya Katiba yanayohusu masharti ya kugombea nyadhifa za kisiasa.

Mahakama ilimwagiza kupata ushauri wa Mwanasheria Mkuu ndani ya siku 21.

Bi Oduor alisema kesi hiyo haifai kuendelea kwa sababu inahusu maswali yenye msingi na huenda ikaathiri kesi za baadaye.

“Afisi hii inaona kwamba kesi hii haikidhi masharti ya Katiba ya Mahakama ya Juu kutoa ushauri wa aina hii,” akasema.

Hata hivyo, mawakili wa Bw Bundi wanasisitiza kuwa Mwanasheria Mkuu hakutimiza maagizo ya mahakama kwa sababu hakujibu maswali muhimu.

Kwa sasa, Mahakama ya Juu bado haijatoa uamuzi kuhusu suala hilo. Hii inaacha swali la iwapo Gachagua na Mwangaza wanaweza kugombea uchaguzi wa 2027 likiwa halijajibiwa.