Maafisa waagizwa kupigia debe mafanikio ya serikali kuelekea 2027
SERIKALI ya Rais William Ruto imeanza kuimarisha kampeni ya mawasiliano kwa umma kuhusu sera, miradi na mafanikio yake huku uchaguzi mkuu wa 2027 ukikaribia.
Hatua hiyo inafuatia barua ya Mkuu wa Utumishi wa Umma na Wafanyakazi wa Ikulu, Felix Koskei, kwa mawaziri, makatibu, msemaji wa serikali na wakuu wa mashirika ya serikali.
Katika barua iliyoandikwa Agosti 17, 2026, Bw Koskei aliwaagiza maafisa hao kuwasiliana moja kwa moja na wananchi na kuelezea juhudi za serikali, sera zake na miradi inayotekelezwa.
“Kuna haja ya dharura ya kuwasiliana kikamilifu na wananchi kwa wakati kuhusu sera, mipango na shughuli muhimu za serikali,” alisema katika barua hiyo.
Hatua hiyo inajiri mwaka mmoja kabla ya uchaguzi wa 2027, huku serikali na upinzani tayari zikianza kujipanga kisiasa.
Ingawa barua hiyo haitaji uchaguzi au kampeni, muda wake umeibua maswali kuhusu nafasi ya mawasiliano ya serikali katika uchaguzi ujao.
Kwa miaka minne iliyopita, serikali imekuwa ikikosolewa kuhusu gharama ya maisha, ushuru, deni la taifa, mageuzi katika afya, makazi, elimu na ukosefu wa ajira.
Upinzani nao umefanya rekodi ya serikali katika uchumi kuwa hoja kuu katika juhudi za kumng’oa Rais Ruto madarakani.
Bw Koskei alisema serikali imekuwa ikijibu masuala yanapozuka badala ya kutoa taarifa kwa wananchi mapema. Wakati mwingine, alisema, maafisa wa serikali wamekuwa wakitoa taarifa zinazokinzana.
Hali hiyo, kulingana na barua hiyo, imechangia kupungua kwa imani ya wananchi kwa serikali.
Sasa kila wizara, idara na shirika la serikali litaandaa mkakati wa mawasiliano unaoendana na Sera ya Kitaifa ya Mawasiliano iliyoidhinishwa na Baraza la Mawaziri.
Mikakati hiyo itahusisha kueleza sera na miradi, namna ya kushughulikia majanga na dharura, kushirikisha wananchi, kutenga fedha za mawasiliano na kuwasiliana mara kwa mara na vyombo vya habari.
Mawaziri, makatibu na wakuu wa mashirika pia wameagizwa kuchukua “jukumu kamili” la kutoa taarifa kwa wakati na kwa njia iliyoratibiwa.
Aidha, wameagizwa kukabiliana na taarifa potovu na kuzuia watu wengine kutawala mjadala wa kitaifa.
Katika enzi ya mitandao ya kijamii, serikali inaonekana kuongeza nguvu katika simulizi kuhusu utendaji wake.
Kituo cha Kitaifa cha Mawasiliano pia kitaanza kutekeleza majukumu yake mara moja.
Kituo hicho, kilichoanzishwa kupitia Amri ya Rais nambari moja ya mwaka 2025, kitatumika kama hifadhi kuu ya taarifa za serikali.
Kituo hicho kitakusanya, kuchambua, kuthibitisha na kuandaa taarifa kabla ya kusambazwa kwa wananchi.
Msemaji wa Serikali Charles Owino atakuwa na jukumu la kusambaza taarifa hizo kupitia majukwaa mbalimbali.
Serikali inataka mawasiliano yake yawe na “uwiano, uthabiti na ufanisi” ili kuzuia taasisi zake kutoa ujumbe unaokinzana.
Miradi mikubwa ya serikali pia italazimika kuwa na mpango wa mawasiliano tangu hatua ya kuandaliwa kwake.
Hii ina maana kuwa miradi kama barabara, hospitali, nyumba za bei nafuu, maji na mipango ya elimu itapaswa kuelekezwa kwa wananchi kuhusu maendeleo yake na manufaa yanayotarajiwa.
Mawasiliano hayo pia yataingizwa katika mikataba ya utendakazi ya maafisa wakuu, hivyo kuwafanya kuwajibika moja kwa moja kwa taarifa wanazotoa kuhusu kazi za serikali.
Majukwaa yatakayotumika ni pamoja na Kenya Broadcasting Corporation, Kenya News Agency, Kenya Yearbook Editorial Board, Government Advertising Agency, tovuti za serikali na mitandao rasmi ya kijamii.
Serikali pia imeagiza matumizi zaidi ya simu za mkononi na majukwaa kama X, Facebook, TikTok, YouTube na WhatsApp.
Hata hivyo, wakosoaji wanaweza kuhoji iwapo hatua hiyo itatumika kutoa taarifa kwa umma au kubadilika na kuwa kampeni inayolipiwa na walipa kodi.
Wakili Chris Omore alisema sheria za uchaguzi na mfumo wa matumizi ya fedha za umma zinaweka mipaka kuhusu matumizi ya rasilimali za serikali kwa shughuli za kisiasa.
“Mawasiliano ya serikali lazima yabaki kutoa taarifa halali kwa umma na yasivuke mpaka na kuwa kampeni ya moja kwa moja ya kisiasa,” alisema.