Habari za Kitaifa

Magenge ya wahuni sasa yawinda wanasiasa na viongozi katika mikutano ya kisiasa

Na TITUS OMINDE June 17th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MIKUTANO ya kisiasa nchini inazidi kuwa uwanja wa mawindo kwa magenge ya wahalifu wa kulipwa, huku wanasiasa, viongozi wa hadhi ya juu na timu zao za kampeni wakilengwa kwa wizi na uporaji.

Mashirika ya usalama yameonya kuwa magenge ambayo hapo awali yalijulikana kwa kufuata misafara ya viongozi wa kisiasa na kudai pesa za kampeni sasa yamebadilika na kuwa mitandao ya uhalifu iliyojipanga vyema.

Makundi hayo hutumia vurugu na msisimko wa mikutano ya kisiasa kuwaibia viongozi na wasaidizi wao fedha, simu za mkononi, vito na mali nyingine za thamani.

Maafisa wa usalama wanasema hali hiyo inatia wasiwasi mkubwa. Katika eneo la North Rift, hasa.

Kaunti ya Uasin Gishu, tatizo hilo limeongezeka kiasi kwamba mamlaka sasa zinachukulia kama tishio kubwa kwa usalama huku shughuli za kisiasa zikitarajiwa kushika kasi kutokana na miungano na mabadiliko ya kisiasa yanayoendelea.

“Tunakumbwa na changamoto ya ongezeko la wahuni wanaoning’inia magari ya viongozi wakuu wakidai motisha zisizo halali,” alionya Kamishna wa Kaunti ya Uasin Gishu, Dkt Eddyson Nyale.

Hata hivyo, maafisa wa usalama wanasema tatizo hilo si la vijana wanaotafuta pesa pekee.

Uchunguzi unaonyesha kuwa baadhi ya magenge huingia katika mikutano ya kisiasa yakijifanya wafuasi au walinzi binafsi wa viongozi maarufu.

Wakiwa ndani ya umati, hutumia msongamano unaotokana na kuwasili kwa viongozi kutekeleza wizi.

Akizungumza katika mkutano wa umma eneo la Tarakwa, Kaunti Ndogo ya Kesses, Dkt Nyale alisema utawala wa eneo hilo hautavumilia tena ongezeko la vitendo vya kihuni.

“Hatutakaa na kukunja mikono huku wazururaji na wahuni wakiendelea kujihusisha na shughuli za uhalifu,” alisema.

Aliongeza kuwa kile kinachoonekana kama shamrashamra za kawaida za kuwakaribisha viongozi sasa kimekuwa maficho ya wahalifu.

“Kuning’inia magari yanayoendeshwa si kosa la trafiki na hatari kwa usalama pekee, bali pia kumekuwa njia ya kutekeleza uporaji na unyang’anyi. Tumeagiza polisi kuwakamata wote watakaopatikana wakizunguka au kuning’inia kwenye misafara ya viongozi wa kisiasa,” alisema.

Kwa mujibu wa Kamishna huyo, taarifa za kijasusi zinaonyesha baadhi ya vijana hao huandaliwa na wanasiasa hasimu kuvuruga mikutano au kuonyesha kana kwamba wanaungwa mkono kwa wingi.

Hata hivyo, wengi wao sasa wamegeuza mikutano hiyo kuwa fursa ya kutekeleza wizi.

Onyo hilo linajiri huku kukiwa na hofu kuhusu kurejea kwa siasa za kutumia wahuni katika maeneo mbalimbali nchini.

Katika wiki za hivi karibuni, video kutoka mikutano ya kisiasa katika kaunti za Uasin Gishu, Trans Nzoia na Nandi zimeonyesha makundi ya vijana yakizingira kwa fujo magari ya viongozi, wakining’inia misafara inayosonga, wakifungua milango kwa nguvu na kusukumana karibu na viongozi wakidai wanawakaribisha.

Baadhi ya viongozi tayari wameathirika. Mwezi Mei, Mbunge wa Mogotio Reuben Kiborek alifichua hadharani kuwa simu yake ya mkononi iliibwa alipohudhuria mazishi ya babake Waziri wa Barabara na Uchukuzi, Davis Chirchir katika Kaunti ya Bomet.

Baadaye mbunge huyo aliandika kwenye mitandao ya kijamii akiwaomba walioiba simu hiyo wamrudishie.

“Lakini watu wa Bomet, mbona mniibie simu na vile nyinyi ni watu wangu. Sharp boys,” aliandika huku akiwaita washukiwa hao “sharp boys” na hata kuahidi zawadi kwa atakayerudisha simu hiyo.

Maafisa wa usalama wanaamini kuwa wizi huo ni sehemu tu ya mtandao mpana wa uhalifu unaokua sambamba na shughuli za kisiasa.

Dkt Nyale alifichua kuwa baadhi ya magenge hayo pia yamepanua shughuli zao na sasa yanawalenga madereva wa magari ya kibiashara.