Nassir aagiza mpango wa lishe shuleni ukaguliwe baada ya malalamishi kushamiri
GAVANA wa Mombasa, Bw Abdulswamad Nassir, ameagiza ukaguzi wa mpango wake wa lishe kwa wanafunzi wa shule za sekondari za kutwa, uliolenga kupunguza gharama ya karo ya shule kwa wazazi.
Hii ni baada ya wazazi kulalamika kwamba bado wanalipa karo ya juu licha ya mpango huo wa serikali ya kaunti, huku mamia ya wanafunzi wakiendelea kufukuzwa shule kwa kutolipa karo.
Bw Nassir ameagiza maafisa wa kaunti kuanza ukaguzi wa mpango huo ili kubaini ukweli.
Maafisa hao watawahoji wazazi, wanafunzi, walimu na wasimamizi wa shule hizo ili kutathmini utekelezaji wa mpango huo.
Zoezi hilo, linalotarajiwa kuanza wiki hii, linalenga kubaini iwapo mpango huo unafanikisha malengo ya kuboresha sekta hiyo na kupunguza gharama za masomo ya sekondari.
Bw Nassir alisema anataka kupata maoni ya moja kwa moja kutoka kwa walengwa.
Chini ya mpango huo, wanafunzi wa shule za sekondari za kutwa hupatiwa chakula kinachofadhiliwa na serikali ya kaunti, huku gharama ya ada ikitarajiwa kushuka kutoka Sh22,000 hadi Sh12,000 kwa mwaka.
“Tulipoanzisha mpango huu, lengo lilikuwa kuboresha elimu na kuhakikisha watoto wanapata lishe bora na kupunguza mzigo wa kifedha kwa familia kwa takriban Sh12,000 kwa kila mwanafunzi kwa mwaka. Sasa tunataka kubaini hali halisi,” alisema.
Alitoa wito kwa wazazi, wanafunzi na wadau wa elimu kushirikiana na serikali yake ya kaunti kutoa maoni ya kweli kuhusu mafanikio na changamoto za mpango huo.