Mkewe Uhuru, nduguze 3 wavutania mali na mjane wa kaka yao mdogo
ALIYEKUWA Mama wa Taifa Margaret Kenyatta amejitosa katika mzozo wa kisheria kuhusu urithi wa mali ya ndugu yake marehemu, William Gakuo Njuguna, akishirikiana na ndugu zake watatu kupinga mjane wa marehemu kuhusu usimamizi wa mali hiyo.
Bi Margaret Kenyatta pamoja na Peter Maina Gakuo, Gabriella Njeri Gakuo na Christine Wambui Gakuo, wanataka Mahakama Kuu kubatilisha hati ya usimamizi wa mali iliyotolewa kwa mjane wa marehemu, Sheila Wanjiku Mwangi, wakidai ilipatikana kwa njia ya udanganyifu na kwa kuficha taarifa muhimu.
Wanadai kuwa mahakama haikufahamishwa kwamba wao ni baadhi ya ndugu wa karibu waliobaki wa marehemu na hivyo walinyimwa nafasi ya kushiriki katika mchakato wa urithi.
Hata hivyo, wakili wa Bi Mwangi, Bw Erick Mutua, amepinga madai hayo akisema ndugu hao hawana haki ya kisheria ya kurithi mali hiyo chini ya Sheria ya Urithi.
Bw William Gakuo Njuguna, mdogo wa Bi Kenyatta, alifariki mnamo Novemba 2024 nyumbani kwake Karen, Nairobi akiwa na umri wa miaka 48.
Stakabadhi za mahakama zinaonyesha kuwa alikufa bila kuacha watoto.
Mali yake inajumuisha ardhi Kaunti ya Narok, hisa katika kampuni za Siaya Greens Limited, Tinderet Greens Limited na Kenindia Assurance Company Limited, gari aina ya Mitsubishi Pajero pamoja na mgao kutoka kwa mali ya marehemu babake, Ephantus Gakuo.
Mali hiyo inakadiriwa kuwa ya thamani ya Sh50 milioni.
Bi Mwangi aliomba Mahakama Kuu apewe mamlaka ya kusimamia mali hiyo akijitambulisha kama mke wa marehemu na mrithi pekee aliyebaki.
Hati hiyo ilitolewa Desemba 2025.
Lakini Peter Maina Gakuo, kwa niaba ya ndugu zake, ameomba hati hiyo ifutiliwe mbali, akisema ilipatikana kwa kuficha ukweli kuhusu watu wengine waliokuwa hai na wenye maslahi katika urithi huo.
“Barua ya usimamizi ilipatikana kwa njia ya udanganyifu kupitia kufichwa kwa makusudi kwa taarifa muhimu kuhusu watu waliobaki baada ya kifo cha marehemu,” walieleza katika maombi yao.
Bi Mwangi amekanusha madai hayo, akisema walalamishi hawakuwa wakitegemea marehemu kwa mujibu wa Sheria ya Urithi na hivyo hakuhitajika kuwataja katika ombi lake.
Katika hati yake ya kiapo ya kujibu kesi, alisema waombaji hao hawajathibitisha kuwa wana haki yoyote ya kisheria, walikuwa wakimtegemea marehemu au kulikuwa na udanganyifu katika mchakato huo.
“Mbali na kukosoa namna ombi lilivyowasilishwa, hawajaonyesha kuwa wana haki yoyote ya kunufaika na mali ya marehemu,” alisema.
Aidha alibainisha kuwa ndugu hao ni watu wazima wanaojitegemea kifedha, akitaja kuwa Margaret Kenyatta ni mke wa Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta.
Wakili Erick Mutua aliunga mkono msimamo wa mjane huyo, akisema ombi la kubatilisha hati hiyo halina msingi wa kisheria na limewasilishwa kwa nia mbaya ili kuendeleza maslahi katika mgogoro mwingine tofauti.
Wakati huo huo, Bi Mwangi amedai kuwa amefungiwa nje ya nyumba yake ya ndoa iliyoko Karen na kunyimwa nafasi ya kuchukua nguo na mali zake binafsi. Pia anadai mfanyakazi wake wa bustani alifukuzwa kwa nguvu.
Katika madai mengine mazito, alisema mumewe alijitoa uhai kutokana na msongo wa mawazo uliotokana na kutopata sehemu yake ya urithi wa mali ya babake, Ephantus Gakuo.
“Alijihisi kutengwa na kuvunjika moyo kwa kuwa alikuwa mtoto pekee wa mama tofauti na waombaji, hali iliyomfanya kuamua kujiua Novemba 7, 2024,” alidai.
Bi Mwangi pia amewashutumu wasimamizi wa mali ya marehemu Ephantus Gakuo kwa kushindwa kutoa maelezo kuhusu takriban Sh300 milioni zilizopatikana kutokana na mauzo ya ardhi katika eneo la Bamburi North kwa serikali, madai ambayo bado hayajathibitishwa mahakamani.
Kesi hiyo itatajwa tena Novemba 2, 2026.