Habari za Kitaifa

Mbunge Amerika apinga mpango wa Trump kujenga kituo cha Ebola Kenya

Na DAVID MONDA June 4th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MBUNGE mmoja nchini Amerika amepinga vikali mpango wa Rais Donald Trump wa kuwaleta Kenya raia wa Amerika walioambukizwa virusi vya Ebola kutengwa na kutibiwa, akisema Amerika ina uwezo wa kuwahudumia wagonjwa hao katika vituo vyake.

Mbunge Gregory Meeks, ambaye ni mwanachama mkuu wa chama cha Democratic katika Kamati ya Masuala ya Kigeni ya Bunge la Amerika, alisema serikali ya Washington inapaswa kuwajibikia raia wake badala ya kuhamishia jukumu hilo kwa Kenya.

“Kuna vituo maalumu nchini Amerika vilivyoundwa kushughulikia wagonjwa wa Ebola kwa usalama. Serikali ya Trump inapaswa kuwaleta Wamarekani hao nyumbani na kuwahudumia badala ya kuhamishia jukumu hilo kwa serikali nyingine,” alisema Meeks kupitia ukurasa wa Kamati ya Masuala ya Kigeni ya chama cha Democratic katika mtandao wa X.

Meeks pia alihoji hatua ya kuomba Kenya iwahifadhi wagonjwa hao huku Amerika ikiwa imepunguza kwa kiasi kikubwa ufadhili wa sekta ya afya nchini Kenya.

Kauli yake inajiri huku ripoti za vyombo vya habari vya Amerika zikidai kuwa maafisa wa Amerika tayari wamewasili katika Kituo cha Jeshi la Anga cha Laikipia. Mbunge huyo alilaumu utawala wa Trump kwa kile alichokitaja kama kudhoofisha mifumo ya afya duniani kupitia kupunguzwa kwa ufadhili wa afya na misaada ya kimataifa.

“Trump na Rubio walivunja USAID, wakapunguza ufadhili wa mipango ya afya duniani na kuondoa Amerika katika Shirika la Afya Duniani (WHO),” alisema.

Mpango huo umeibua maoni tofauti miongoni mwa Wakenya wanaoishi Amerika Profesa Kefa Otiso wa Chuo Kikuu cha Bowling Green alisema haamini kuwa kituo hicho kitaongeza hatari ya Ebola nchini Kenya, akieleza kuwa nchi tayari imewahi kuanzisha vituo vya maandalizi dhidi ya ugonjwa huo.

“Mapema au baadaye, Ebola itafika Kenya tu,” alisema.