Habari Mseto

Mama mkarimu auawa na aliyempa maji ya kunywa

Na DAVID MUCHUI August 19th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

HUZUNI na mshtuko zimetanda katika kijiji cha Chabuene, Kaunti ya Meru, kufuatia mauaji ya kikatili ya Evelyne Mukiri Mbaabu, mwanamke anayekumbukwa kwa ukarimu wake na juhudi zake za kuhifadhi mazingira.

Mkasa huo ulitokea mnamo Agosti 7 majira ya saa moja usiku, baada ya mwanaume asiyejulikana kuingia nyumbani kwake akiomba maji ya kunywa.

Kwa mujibu wa familia, Bi Mukiri, mwenye umri wa miaka 65, alimkaribisha mgeni huyo na hata kumualika kwa kula chakula cha jioni.

Kisha akamtuma mjukuu wake kwenda kuchota maji kutoka nyumba kuu huku akiendelea kuandaa chakula katika jiko lililojengwa nje ya nyumba.

Hata hivyo, muda mfupi baadaye ukarimu wake uligeuka kuwa mkasa.

Kwa mujibu wa ripoti ya polisi, mjukuu huyo alipokuwa akichukua maji alisikia mayowe ya nyanya yake.

“Aliporudi mbio jikoni, alimkuta mwathiriwa akiwa amelala katika dimbwi la damu amejeruhiwa,” ilisema ripoti ya polisi.