Mwisho wa ‘nganya’ wanukia korti ikipiga marufuku mapambo ya matatu
MIKE Oby, amekuwa akipamba magari ya huduma ya umma, yanayojulikana kama matatu au nganya, kwa miaka 10 sasa.
Mwanaume huyo mwenye umri wa miaka 39 hufanya kazi na timu, na anasema siku nzuri, hupata kati ya Sh50,000 hadi Sh60,000, huku wengine wakipata kati ya Sh10,000 hadi Sh20,000 kwa kupamba matatu.
Hata hivyo, kufuatia Mahakama Kuu kuidhinisha marufuku katika matatu, sanaa za mapambo na madirisha kwenye matatu, yeye ni miongoni mwa Wakenya wanaokabiliwa na ukosefu wa ajira.
“Kwa marufuku hii, wasanii na wabunifu wanaofanya mapambo na kazi zote hizo watakosa kazi,” anasema.
Bw Oby anasema kubadilisha matatu moja huendesha maisha ya Wakenya wengi, kuanzia mafundi, wachoraji, mafundi wa umeme, wabunifu wa ndani na wengine. Watu 5 hadi 10 huandaa matatu kwa kupaka rangi.
Kisha wasanii huingia, wakati mwingine watano au sita, kuchora mapambo. Baadaye fundi wa taa na mfumo wa burudani hufuata, na hatimaye madereva na makondakta huchukua nafasi.
“Katika matatu moja, tunahitaji timu ya watu takriban 50,” anasema.
“Fikiria watu 50 wakipoteza kazi zao.”
Si wasanii pekee wanaoathirika; wauzaji wa rangi na vifaa vya taa pia wamekuwa wakinufaika na biashara hii.
Baadhi ya wauzaji wanasema wamekuwa wakitoa bidhaa kwa mkopo wakitarajia kulipwa baada ya wamiliki kumaliza malipo. Bw Oby anasema wateja wengi sasa wamesitisha miradi wakisubiri mwelekeo wa uamuzi huo.
Anasema marufuku hii si haki. “Ajali ikitokea sio mapambo husababisha, ni dereva,” anasema.
“Adhabu iwe kwa dereva, si sanaa.”
Babel Gody, 31, mbunifu mwingine jijini Nairobi anasema matatu iliyopambwa si mapambo tu bali utamaduni wa jiji.
“Michoro kwenye matatu huzipatia upekee,” anasema.
Yeye pia amesitisha miradi karibu mitatu kutokana na sintofahamu hiyo. Anasema karibu asilimia 70 ya watu kwenye sekta hiyo wanaweza kupoteza ajira.
“Waliotoa marufuku walipaswa kuja kuona uhalisia,” anasema.
Patrick Kimweli, 30, hajawahi kufanya kazi nyingine zaidi ya sanaa ya matatu. Alianza baada ya kumaliza shule ya upili.
“Nilijikita hapa tu,” anasema.
Kwa siku za kawaida hupata Sh5,000 hadi Sh6,000, lakini sasa miradi mitatu imesimama.
“Wateja wanapiga simu wakiwa wamekasirika,” anasema.
Anasema sanaa ni tiba kwake. “Nikiwa na huzuni, kuchora hunipa amani.”
Baadhi ya viongozi wanasema uamuzi huo unahatarisha uhuru wa kujieleza na sekta ya ubunifu.
Mbunge wa Lang’ata Felix Oduor (Jalang’o) amesema atasimamia gharama za rufaa mahakamani, akisema nganya ni utamaduni wa Nairobi.
Seneta Samson Cherargei amesema marufuku hiyo ni tishio kwa uhuru wa kujieleza na tasnia ya ubunifu.