Raila akubali kushindwa katika uchaguzi wa AUC
MGOMBEAJI wa Kenya wa kiti cha uenyekiti wa Tume ya Muungano wa Afrika (AUC), Raila Odinga, amekubali rasmi kushindwa katika azma yake ya kuongoza muungano huo wa bara, muda mfupi baada ya kushindwa na Waziri wa Masuala ya kigeni wa Djibouti Mahmoud Ali Youssouf.
Bw Youssouf alimshinda Bw Odinga baada ya kupata kura 33 zinazohitajika. Raila alijiondoa baada ya duru ya sita. Katika awamu ya sita, Bw Odinga alikuwa na kura 22, huku Bw Youssouf akiwa na kura 26.
Akizungumza baada ya uchaguzi, Bw Odinga alikubali matokeo ya uchaguzi wa AUC, ambapo alikuwa akishindana na Mahmoud na aliyekuwa Waziri wa Masuala ya kigeni wa Madagascar Richard James Randriamandrato.
“ Nataka kumtakia kila la heri mshindani wangu Mahamoud Ali Youssouf. Namtakia mafanikio katika kazi yake. Ninawashukuru walionipigia kura na wale ambao hawakunipigia kura kwa sababu walitumia haki zao za kidemokrasia,” Bw Odinga alisema, akisindikizwa na maafisa kadhaa wa Kenya waliokuwa wameandamana naye hadi Addis Ababa.
Alisema kukubali kwake kunapaswa kueleweka kama kujitolea kwake kwa demokrasia, akisema, “mimi mwenyewe nilikubali kushindwa. Nataka tutumie hili kama mfano wa kuimarisha demokrasia katika bara letu.”
Bw Odinga alitafakari kuhusu kampeni ya miezi kadhaa ambayo ilimfanya kusafiri kote barani Afrika kuomba kura.
“Nilijitolea kama mgombeaji, na katika miezi michache iliyopita, nimezunguka bara nikizungumza na viongozi, nikitafuta kura zao. Leo wamezungumza. Na kama ilivyo sasa, hatukufanikiwa,” alisema na kuongeza kuwa hatajali kutoa huduma zake kwa bara wakati wowote akiitwa.
Akizungumzia changamoto pana zinazokabili Afrika, Bw Odinga aligusia mzozo unaoendelea katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC). “Suala la DRC linasalia kuwa suala tata. Aina ya mateso tunayoona haikubaliki kabisa. Wanaua watu wasio na hatia, watoto, wanawake na kadhalika. Ni lazima ikomeshwe,” alisema, akionyesha hitaji la suluhu kwa dharura.
Alipoulizwa kuhusu hatua zake zinazofuata, Odinga alibaki na matumaini, akisema, “Unapoenda kwenye mashindano, kunaweza tu kuwa na matokeo mawili. Unaweza kushinda, au unaweza kushindwa. Sina uchungu. Nimefurahia sana, kwa kweli. Na bado niko tayari kutoa huduma kwa bara katika nafasi nyingine yoyote.
Waziri Mkuu huyo wa zamani alimalizia kwa kutoa shukrani zake kwa watu wa Afrika kwa kusema, “Nawashukuru wananchi. Nawashukuru watu wa Afrika. Viva Afrika!”