• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 1:22 PM
Utafiti wafichua nusu ya Wakenya waamini nchi inaelekea pabaya

Utafiti wafichua nusu ya Wakenya waamini nchi inaelekea pabaya


Na NDUBI MOTURI

ZAIDI ya nusu ya Wakenya wanaamini kuwa nchi inaelekea vibaya, utafiti wa kampuni ya Infotrak umeonyesha.

Ni asilimia 19 pekee ya Wakenya wanaoamini kuwa, nchi inaendeshwa vyema huku wengi wakitaja gharama ya maisha kama sababu ya nchi kuelekea vibaya.

“Idadi ya Wakenya ambao walitaja gharama ya juu ya maisha kama suala kuu linaloibua wasiwasi iliongezeka kutoka asilimia 56 mnamo Desemba 2023 hadi asilimia 58 Machi 2024,” ulisema utafiti huo.

Iliyokuwa mikoa ya Pwani, Nyanza na Magharibi ndio ina idadi kubwa zaidi ya Wakenya wanaoamini nchi inaelekea pabaya kwa asilimia 70, 68 na 64 mtawalia.

Kwa upande mwingine, Wakenya wanaoishi katika maeneo ya Bonde la Ufa na Nairobi wanachangia asilimia kubwa zaidi ya wale wanaoamini kuwa nchi inaendeshwa vyema kwa asilimia 32 na 21 mtawalia.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa ripoti ya utafiti huo, meneja mkuu wa shughuli za nyanjani wa Infotrak, Johvine Wanyingo alisema gharama ya juu ya maisha na utozwaji ushuru mkubwa ni masuala makuu yanayotia Wakenya wasiwasi.

Wanaoamini kuwa nchi inaelekea pazuri walitaja sababu kuu ya kuwepo kwa amani nchini.

“Kumekuwa na amani nchini kwa muda. Kura ya maoni hata hivyo ilifanywa wakati mgomo wa daktari ulikuwa haujaanza na matokeo yangekuwa tofauti sana,” alisema.

Wakenya walitaja Seneti na Mahakama kama taasisi wanazoamini zinafanya vyema nchini kwa kupata alama B ya asilimia 69 na 67 mtawalia.

  • Tags

You can share this post!

Kuondoa upigaji msasa katika mchakato wa kutoa vitambulisho...

Mgomo sasa waanza kuathiri kesi zinazohitaji ushahidi wa...

T L