Wakenya kuumia zaidi Sh1.3 trilioni zikitumika kulipia madeni kwenye bajeti ijayo
WAKENYA wataumia zaidi katika mwaka ujao wa kifedha, wa 2026/2027, baada ya serikali kupanga kutumia Sh1.3 trilioni za bajeti ya Sh4.76 trilioni kulipia madeni, kulingana na makadirio yaliyowasilishwa na Hazina ya Kitaifa bungeni Aprili 30, 2026.
Matumizi ya kiasi kikubwa kama hicho cha pesa kulipia madeni, kutapunguza mgao wa fedha kwa miradi ya maendeleo itakayozalisha nafasi ya ajira.
Bajeti ya mwaka ujao wa kifedha iko juu ikilinganishwa na bajeti ya mwaka wa kifedha wa sasa ambao ni Sh4.6 trilioni.
Aidha, inazidi kiwango kilichoko katika Taarifa ya Sera ya Bajeti (BPS) iliyopitishwa na Bunge la Kitaifa mnamo Machi mwaka huu, kwa Sh64 bilioni.
Ikiwa bajeti ijayo, ya Sh4.76 trilioni, itapitishwa na Bunge la Kitaifa ilivyo kwenye makadirio yaliyoko bungeni wakati huu, serikali ya kitaifa itapata Sh2.9 trilioni.
Mgao huo unajumuisha Sh2.82 bilioni zitakazoendea Serikali Kuu, Sh48.7 bilioni zitakazoendea Bunge na Sh30.44 bilioni zitakazotengewa Idara ya Mahakama.
Mgao wa serikali kuu unajumuisha Sh1.98 trilioni za matumizi ya kawaida na Sh840.61 bilioni zitakazotumika katika ufadhili wa miradi ya maendeleo.
Serikali 47 za kaunti nazo zimetengewa Sh420 bilioni za fedha zitakazotokana na ushuru utakaokusanywa na serikali ya kitaifa.
Nayo serikali kuu inakadiria kukusanya mapato ya kima cha Sh3.63 trilioni kutokana na ushuru na kupokea Sh644 bilioni kama misaada kutoka ng’ambo, ikisalia na upungufu wa Sh1.11 trilioni.
Upungufu huo utajazwa kupitia ukopeshaji Sh995.7 bilioni kutoka mashirika ya kifedha ya humu nchini na Sh145.6 bilioni kutoka nje ya nchi.
Mgao wa fedha za kulipia madeni uko chini ya Hazina ya Huduma za Jumla (CFS) ambazo pia zinajumuisha Sh247.1 bilioni za malipo ya pensheni na mishahara ya Maafisa Wakuu wa Serikali.
Waziri wa Fedha John Mbadi anasema makadirio hayo yalitayarishwa kwa lengo la kudumisha uthabiti wa kiuchumi kwa kudhibiti mfumko wa bei na kudumisha fedha za kutosha za kigeni za hadi miezi mitano.
Aidha, alisema makadirio hayo yametayarishwa kwa lengo la kuongeza kiwango cha ukusanyaji mapato kupitia ushuru.
“Serikali inalenga kupunguza pengo katika bajeti hadi kima cha asilimia 4.1 ya Jumla ya Mapato ya Taifa (GDP) huku ikidumisha usawa katika ukopeshaji kutoka humu nchini na nje,” anasema Bw Mbadi.
Maelezo kutoka kwa Afisi ya Mdhibiti wa Bajeti (CoB) yanaonyesha kuwa kiwango cha deni la kitaifa ni Sh12.29 trilioni.
Hata hivyo, kupungua kwa kiwango cha mapato kunakotarajiwa, jinsi kulivyoshuhudiwa katika miaka ya kifedha iliyopita, kunaashiria kuwa serikali itaendelea kukopa kutoka mashirika ya kifedha nchini ili kugharamia shughuli zake.
Hata hivyo, Waziri Mbadi anasema juhudi zitaweka kuimarisha mifumo ya usimamizi wa fedha za umma, ili kuhakikisha kuwa fedha zinatumika kwa mipango na miradi yenye umuhimu kwa umma pekee.