Polisi wachunguza mhadarati wa ‘Karambela’ unaodaiwa kugeuza waraibu machizi na wauaji
ONGEZEKO la matumizi ya dawa mpya za kulevya kwa jina la mtaani ‘Karambela’ linazidi kutia hofu jamii za Pwani, hasa Lamu.
Mihadarati hiyo imelaumiwa kwa kuchangia mauaji ya kinyama yanayotekelezwa na waraibu wanaotumia mapanga, maarufu ‘Panga Boys.’
Punde wanapotumia Karambela huishia kugeuzwa wenye kuzua vurugu bila woga.
Katika kipindi cha miezi mitatu iliyopita, Lamu imeshuhudia vifo vya zaidi ya vijana 10 ilhali wengine wakiachwa na majeraha mabaya kupitia uvamizi wa mapanga.
Maeneo yaliyorekodi visa hivyo ni kisiwa cha Lamu, Mokowe, Faza, Kizingitini, Mbwajumwali na viunga vyake.
Katika mahojiano na Taifa Leo Jumatatu, Naibu Gavana wa Lamu, ambaye pia ni Waziri wa Afya wa kaunti hiyo, Dkt Mbarak Salim alilinganisha Karambela na dawa inayotambulika kama ‘Benzodiazepine.’
Benzodiazepine ni kundi la dawa zinazotumika kutibu matatizo mbalimbali kama vile wasiwasi mkubwa na matatizo ya kukosa usingizi.
Pia, ni dawa zinazotumika kutuliza mfumo mkubwa wa neva.
“Hiyo Karambela ninaifananisha na Benzodiazepine kutokana na athari zinazoonekana kwa anayezitumia. Wanazitumia vibaya, hivyo kuwapa nguvu na ujasiri wa kutekeleza vitendo ambavyo kwa kawaida na wakiwa macho makavu hawawezi kuvifanya, ikiwemo kumkata mtu kwa upanga na kumuua,” akasema Dkt Salim.
Mihadarati hiyo ya Karambela inaaminika kutengenezwa kienyeji kutoka nchi jirani ya Somalia.
“Wanaunda hiyo dawa na mchanganyiko sawia na kisha kuziweka kwenye paketi kana kwamba ni dawa aina ya Diazepam. Ziko rangi ya samawati. Wanaonunua na kuzitumia vibaya huishia kutekeleza vitendo visivyo vya kibinadamu,” akasema Dkt Salim.
Kiongozi wa Vijana Lamu, Bw Fuad Ali anasema waraibu hutumia kati ya vidonge 10 au 20 vya Karambela.
Kulingana na Bw Ali, dawa hizo hununuliwa kiurahisi kwenye maduka ya uchuuzi au yale ya dawa.
Anafafanua kuwa punde wahusika wanapozitumia vibaya huchanganyikiwa kiakili.
“Wanaanza kufikiria visivyokuwepo. Mwishowe unawapata wamefanya vitendo vya kinyama, ikiwemo kuua wengine kwa mapanga katika kulipizana visasi,” akasema Bw Ali.
Kiongozi huyo wa vijana alikashifu bodi zinazohusika na usambazaji na udhibiti wa dawa na sumu nchini kwa utepetevu.
“Utaachiliaje dawa ambazo hazifai kuendelea kusambazwa na kuuzwa kiholela madukani mitaani? Lazima bodi husika zishirikiane na polisi na kutekeleza misako ya kushtukiza kwenye haya maduka ya dawa na mitaani kunasa hizo Karambela na wahusika wa biashara hiyo,” akasema Bw Ali.
Maafisa wa utawala waliohojiwa na Taifa Leo na kudinda kutaja majina yao waliwalaumu wachuuzi wa miraa kwamagari barabarani na boti baharini kwa kuingiza kisiri karambela Lamu na Pwani.
“Hiyo Karambela unayosikia inatoka Isiolo na Somalia. Inaingizwa Lamu kupitia barabara zetu na uchukuzi wa baharini. Lazima wazifanyie upekuzi gari na boti za miraa. Hao ndio wanaopenyeza hiyo Karambela Pwani na Lamu,” akasema mmoja wa maafisa.
Kamanda wa polisi kaunti ya Lamu, Bw Shadrack Ruto aliwaonya wamiliki wa maduka ya dawa dhidi ya kuwauzia waraibu vidonge hivyo vya Karambela bila maelekezo ya daktari.
“Tunajua kuna mihadarati hatari kwa jina Karambela inayouziwa vijana waraibu wa mihadarati hapa Lamu. Wanapotumiwa wanageuzwa wanyama, hivyo kuwakata na kuwaua wengine kwa mapanga. Tunachunguza na tutawashika wahusika,” akasema Bw Ruto