Habari

Huzuni watu 15 wakiaga kwenye mgodi West Pokot

Na TITUS OMINDE na BARNABAS BII May 9th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MAWE makubwa yaliporomoka ghafla kutoka milima ya Ramos iliyo na madini katika eneo la Kasei, Kaunti ya West Pokot, na kubingiria kuelekea mahali ambapo wachimbaji wa dhahabu walikuwa karibu na migodi na kuua 15.
Mawe hayo yaliwagonga baadhi papo hapo na kuwazika wengine wakiwa hai chini ya vifusi na migodi iliyoporomoka pia.
Walioshuhudia walisema wachimbaji hao, wakiwemo wanawake waliokuwa wakisafisha madini karibu na migodi, hawakuwa na nafasi ya kutoroka wakati mawe hayo yaliposhuka kwa kasi na kufunika eneo lote, yakiziba mashimo kadhaa na kuwanasa wachimbaji waliokuwa chini ya ardhi.
“Waathiriwa walikuwa wakisubiri dhahabu ipandishwe juu kwa kusafishwa wakati mawe yalipoteremka ghafla kutoka mlimani na kuwazika wakiwa hai ndani ya mashimo,” alisema chifu wa eneo la Lopet, Isaac Lomwai.
Takriban wachimbaji 15 — wanawake 12 na wanaume watatu— walithibitishwa kufariki katika mkasa huo wa Alhamisi, kulingana na duru mbalimbali za eneo hilo, huku timu za uokoaji zikiendelea kupekua vifusi kwa hofu kuwa huenda wengine bado wamegubikwa chini ya ardhi. Taarifa za awali zinaonyesha kuwa, shughuli za uchimbaji zilizoshamiri huenda zilidhoofisha udongo ulioshikilia miamba, hali iliyochochea maporomoko hayo hatari.
Kamishna wa Kaunti ya Pokot Magharibi Daniel Saruni alisema alikuwa akielekea eneo la tukio kufanya tathmini kabla ya kutoa taarifa kamili.
“Ninaelekea eneo la tukio kutathmini hali kabla ya kutoa taarifa kamili,” alisema kwa simu.
Wachimbaji waliojeruhiwa walikimbizwa katika Zahanati ya Turkwel, huku walio katika hali mbaya zaidi wakipelekwa katika Hospitali ya Rufaa ya Kapenguria kwa matibabu maalumu.
“Tulipokea wachimbaji watano waliojeruhiwa, wawili kati yao wakiwa mahututi na tulilazimika kuwafanyia upasuaji,” alisema msimamizi wa hospitali hiyo, Dkt Simon Kaplongit Kapchanga.
Alisema majeruhi walivunjika mikono na miguu vibaya, wengine wakapata majeraha ya kichwa na maumivu makubwa ya mwili, huku wengine wakihitaji upasuaji au kukatwa viungo.

“Waliolazwa hospitalini Alhamisi usiku ni wanaume wanne na mwanamke mmoja. Wawili walipelekwa moja kwa moja chumba cha upasuaji na sasa wako katika hali nzuri,” alisema Dkt Kapchanga.
Shirika la Msalaba Mwekundu Kenya liliongoza oparesheni za uokoaji huku hofu ikiongezeka kuwa huenda bado kuna watu walio chini ya vifusi.
 “Tumepeleka timu za uokoaji na ufuatiliaji kusaidia kutafuta manusura na kusaidia familia zilizoathirika,” alisema Oscar Okumu, meneja wa Shirika la Msalaba Mwekundu eneo la North Rift.
Alisema hali ya ardhi inazuia juhudi za uokoaji na kuhamisha majeruhi.
“Tumepeleka mifuko ya kuhifadhi miili, na taarifa zinaonyesha kuwa miili bado ipo eneo la tukio,” alisema kwa simu.
Mkasa huo umetokea wiki moja tu baada ya Gavana Simon Kachapin kuonya kuhusu hatua kali za kisheria dhidi ya uchimbaji haramu wa dhahabu kaunti hiyo.
Gavana huyo alishutumu watu wenye ushawishi kwa kufyonza rasilimali za eneo hilo huku wakiharibu mazingira, akisema wakazi wamechoshwa na shughuli hizo haramu zinazoendelea.
 Licha ya vifo vya mara kwa mara katika maeneo ya uchimbaji kama Kambi Karaya, Lami Nyeusi, Morita na Ramos, wakazi bado hurudi katika mashimo hayo hatari kutafuta riziki, mara nyingi wakihatarisha maisha yao.
Mnamo Oktoba 2025, watu wanne akiwemo mtoto wa miaka 14 walifariki baada ya mgodi kuporomoka Kambi Karaya, huku wengine wawili wakiuawa eneo hilo Juni 11, 2025.
Wengine wanne; wanaume watatu na mwanamke mmoja, walifariki na watano kujeruhiwa Juni 7, 2025 baada ya mgodi kuporomoka katika kijiji cha Karon, Turkwel.