Habari

Kesi ya wizi wa magazeti ya kidijitali ya NMG yaanza

Na RICHARD MUNGUTI April 28th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

KESI ambapo mtaalamu wa masuala ya kiteknolojia Antony Mwanzia Kimeu ameshtakiwa kuuza magazeti ya kidijitali ya Kampuni ya Nation Media Group (NMG) PLC ilianza kusikizwa jana huku mkuu wa masuala ya usalama Samuel Koskei akielezea jinsi wizi huo ulivyotekelezwa.

Hakimu mwandamizi wa Mahakama ya Milimani, Nairobi, Teresia Nyagena aliambiwa mshtakiwa akishirikiana na watu wengine, walidungua mtandao wa kidijitali wa NMG kabla ya kuanza kuuza magazeti yake ya Taifa Leo, The Daily Nation, The Business Daily na The East African kati ya Juni 23 na Julai 10, 2025.

Akitoa ushahidi Bw Koskei alieleza mahakama alipokea ujumbe kutoka kwa Mkurugenzi Mkuu wa Masuala ya Fedha, Bw Richard Tobiko kwamba “kulikuwa na walaghai waliokuwa wanauza magazeti ya dijitali ya NMG bila idhini”.

Bw Koskei alisema baada ya kupashwa habari hizo kwa njia ya mtandao wa Whatsapp, aliwasiliana na maafisa wa uhalifu wa kimtandao katika idara ya uchunguzi wa jinai (DCI).

Mkuu huyo wa masuala ya usalama wa vyombo vyote vya NMG alianza uchunguzi pia akishirikisha watalaamu wa kibinafasi -Linswale Risk Management Consultancy Limited.

“Niliwakabidhi wachunguzi wa DCI na Linswale nambari ya simu ambayo ilikuwa ikutumika kudungua magazeti ya NMG na kuwauzia wateja kwa bei rahisi,” Bw Koskei alieleza hakimu Aprili 27, 2026 alipotoa ushahidi.

Bw Koskei alisema nambari ya simu aliyopewa na Bw Tobiko ni nambari 0702976857-iliyokuwa imesajiliwa kwa jina Calvin Kungu.

Hakimu alielezwa Kungu na mshukiwa mwingine walitiwa nguvuni na kushtakiwa.

Hatimaye wawili hawa walimfichua Mwanzia ambaye walisema ndiye alikuwa anawawasambazia magazeti ya kidijitali wauze.

Mahakama iliambiwa magazeti hayo yalikuwa yanauzwa kwa bei ya Sh300.

Shahidi mwingine Stephen Makokha Mukhwana kutoka kwa kampuni ya Linswale alijifanya mnunuzi ndipo akawasiliana na Bw Kungu aliyemwagiza alipie magazeti.

Bw Mukhwana ndiye aliprlrkea Kungu kutiewa nguvuni.

Kesi itaendelea Juni 15 na 16 2026.

Mashahidi kutoka Safaricom watatoa ushahidi.

Mwanzia amekana mashtaka mawili ya kuuza magazeti ya kidijitali ya NMG Plc bila idhini yake.