• Nairobi
  • Last Updated May 4th, 2024 10:15 PM
AfCFTA yazindua programu ya simu kupanua biashara barani Afrika

AfCFTA yazindua programu ya simu kupanua biashara barani Afrika

NA RICHARD MAOSI

BARA la Afrika limepiga hatua muhimu katika ndoto yake ya kuanzisha soko la pamoja la kidijitali baada ya kuzindua programu ya simu hapo Jumanne itakayounganisha wafanyabiashara katika mataifa yote 54.

Hatua hiyo sasa imezidisha juhudi za kuwa na usemi katika soko la kidijitali duniani, huku wajasiriamali barani wakifunguliwa mfumo wa mtandaoni chini ya mpango wa Soko Huru la Africa (AfCFTA), ambao unalenga kuondoa visiki vya biashara mipakani.

Usimamizi wa AfCFTA uliambia Taifa Leo kuwa mradi huo wa kidijtali utawasaidia wafanyabiashara kupata ufadhili wa kifedha kabla na baada ya uzinduzi wa soko hilo hapo Januari Mosi, 2021.

“Kuzinduliwa kwa program hii pamoja na mashindano ya Vision Challenge ili kuwapiga jeki wavumbuzi wetu kufanya bishara barani ni idhibati kuwa kuna uwezo mkubwa na moyo wa kujituma kukuza biashara,” alisema Bw Francis Mangeni, mkurugenzi wa mipango na matangazo katika AfCFTA.

Apu hiyo pia inanuia kumaliza changamoto ya utambulisho wa mitandaoni kwa baadhi ya kampuni na biashara zinapohitajika kufanya hivyo na benki.

Programu hiyo ya simu inaweza kupakuliwa kutoka mtandao wa AfCFTA na itatumika kutoa taarifa muhimu za uwekezaji kwa wafanyabiashara.

Hili linajiri siku chache kabla ya kuandaliwa kwa kongamano la marais wa mataifa ya Afrika hapo Desemba 5, 2020 ambapo masuala muhimu kuhusu mpango mzima wa mradi huo yatajadiliwa.

Mradi huo sasa huenda ukawa fursa kubwa zaidi ya Afrika kujiletea mageuzi ya kimaendeleo, ikizingatiwa unaunda soko kubwa zaidi duniani lenye watu bilioni 1.3, Alitakalokuwa na uwezo wa kutoa ushindani kwa China, India, Ulaya na Amerika.

“Ni kweli kuwa Afrika tayari ina mikataba kadhaa ya kibiashara katika ngazi ya maeneo, lakini AfCFTA ni tofauti kwani imeundwa kufikia ndoto za waliounda wazo la Umoja wa Afrika. Litakuwa soko la hakika lenye uwezo mkubwa wa kushindana na mibabe ya biashara duniani,” aliongeza Bw Mangeni.

Benki kadhaa zikiwamo TDB, Africa50, AfDB, AFC, Equity Bank, Ecobank na Afreximbank zitasaidia katika ufadhili wa AfCFTA Vision Challenge ambapo wajasiriamali mbalimbali barani watajitokeza kuwania tuzo.

Mradi huo ukitekelzwa ipasavyo utapanua biashara baina ya mataifa ya Afrika huku uichangia pakubwa kukuza uchumi wa bara katika sekta mbalimbali.

You can share this post!

TAHARIRI: Wakulima wapewe mawasiliano kisasa

Ufufuzi wa kesi za 2007 wazua maswali