• Nairobi
  • Last Updated April 30th, 2024 5:46 PM
Amerika yataja Wakenya wawili magaidi sugu wa kimataifa

Amerika yataja Wakenya wawili magaidi sugu wa kimataifa

Na KEVIN KELLEY

WIZARA ya Mashauri ya Kigeni ya Amerika imewaorodhesha Wakenya wawili viongozi wa kundi la Al-Shabaab kuwa “magaidi wa kimataifa.”

Hatua hiyo ya kuwalenga Ahmad Iman Ali na Abdifatah Abubakar Abdi inanuia kuwanyima rasilmali zinazohitajika kupanga na kuendesha mashambulizi yao ndani na nje ya Kenya pamoja na Somalia.

Hatua hiyo inalenga kuwazuia wawili hao kupata pesa za kupanga na kutekeleza mashambulizi yoyote ya kigaidi. Pia mali yao yoyote ambayo huenda iko nchini Amerika itazuiliwa na pia raia wa Amerika hawaruhusiwi kufanya nao biashara yoyote.

Ali ameendesha shughuli za Al-shabaab nchini Kenya kwa miaka sita iliyopita na anaaminika kuhusika na vifo vya mamia ya watu.

Wizara hiyo inasema kuwa Ali aliratibu shambulio la Januari 2016 katika kambi ya Jeshi la Kenya ya El Adde ambayo ndiyo tukio baya zaidi la kushindwa kwa jeshi katika historia ya Kenya. Kulingana na Umoja wa Mataifa, takriban wanajeshi 150 wa Kenya waliuawa katika shambulizi hilo.

“Ali pia anawajibika kwa propaganda za Al-Shabaab zinazolenga serikali ya Kenya na rais, kama video ya Julai 2017, ambapo alitoa vitisho kwa Waislamu wanaohudumu katika vikosi vya usalama nchini Kenya,” wizara hiyo ilisema.

Ali alihudumu kama kiongozi wa dini wa kituo cha Muslim Youth Center, Nairobi ambacho mnamo 2012 kilitangaza kuwa kimeungana na Al-Shabaab. Pia alijaribu kuwasajili vijana wa mitaa ya mabanda ya Nairobi kujiunga na kundi hilo.

Naye Abdi anasakwa kuhusiana na mashambulio ya Juni 2014 eneo la Mpeketoni, Kenya ambapo watu zaidi ya 60 waliuawa.

Hatua hiyo ya Alhamisi ya kuwaorodhesha inawanyima Ali na Abdi uwezo wa kufikia mfumo wa kifedha wa Amerika na itasaidia hatua za watekelezaji sheria Amerika na serikali nyingine, wizara hiyo ilisema.

Mbali na kuorodheshwa leo na waziri huyo, Ali na Abdi pia wameorodheshwa katika Kamati ya Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kuhusiana na maafikiano yaliyofanywa kuhusu Somalia na Eritrea.

Kenya, imeshudiwa mashambulio kadha ya kigaidi ambayo ni pamoja na shambulio kubwa zaidi la 1998 lililolenga ubalozi wa Amerika.

You can share this post!

Walimu sasa waacha kutumia vitabu vipya

Mimi ni kigugumizi, Jaji Mwilu afichua kuhusu maisha yake

adminleo