• Nairobi
  • Last Updated May 4th, 2024 1:14 PM
Baktash Akasha ahukumiwa kifungo cha miaka 25 jela Amerika

Baktash Akasha ahukumiwa kifungo cha miaka 25 jela Amerika

Na KEVIN J. KELLEY na CHARLES WASONGA

MAHAKAMA moja ya Amerika imemhukumu Baktash Akasha kifungo cha miaka 25 jela baada ya kumpata na hatia ya kuhusika katika ulanguzi wa mihadarati.

Kiongozi wa jopo la majaji ambao wamekuwa wakisikiza kesi dhidi ya Mkenya huyo, Victor Marrero, pia amemtoza faini ya dola 100,000 (Sh10.3 milioni).

Baktash na kakake mdogo Ibrahim Akasha walishtakiwa kwa kusafirisha tani kadhaa za dawa za kulevya aina ya heroini hadi nchini Amerika.

Walikiri makosa yao na kukubali makosa yao.

Walikubali kuwa walipanga njama ya kuingiza heroini na dawa aina ya methamphetamine nchini Amerika.

Hukumu dhidi ya Ibrahim itasimwa na Jaji Victor Marrero mnamo Novemba 2019.

Kaka hao walichukuliwa nchini Kenya na kusafirishwa hadi Amerika bila familia zao kujulishwa au mawakili wao na licha ya kuwepo kwa agizo la mahakama la kuzuia kusafirishwa kwao hadi Amerika.

Wakati wa kusikizwa kwa kesi hiyo Julai, jaji huyo alisema kuwa amekubaliana na madai yaliyowasilishwa dhidi ya wana hao wa Akasha.

Bunduki

Kaka hao pia walikiri kubeba na kutumia bunduki aina ya machineguns kuendeleza mipango yao ya kuingiza dawa za kulevya nchini Amerika.

Stakabadhi moja iliyowasilishwa kortini mnamo Julai 25, 2019, ilielezea sababu za kuitaka mahakama isitoe hukumu nyepesi kwa kaka hao wa Akasha.

Sababu hizo zinajumuisha madai kwamba Baktash aliua aliyekuwa mkewe, alimtesa mwanawe wa kiume, alikodi wauaji kumwangamiza babake na kuhusika katika shughuli za ulanguzi wa silaha kwa ushirikiano na kundi la kigaidi la al-Shabaab.

“Kaka wa Akasha walilinda biashara ya mihadarati kwa kutumia ukatili, mauaji, vitisho na mikakati yoyote ya kihalifu waliorithi kutoka kwa baba yao aliyeuawa mnamo mwaka wa 2000,” stakabadhi hiyo iliyotolewa na upande wa mashtaka ilisema.

You can share this post!

Kamati nyingine ya upatanisho yabuniwa kujaribu kutanzua...

MAKALA MAALUM: Ubandikaji wa kope bandia ndilo gumzo kuu...

adminleo