Kimataifa

DRC yazima vyombo vya habari kupeperusha habari za Kabila

Na NA MASHIRIKA Tafsiri: CHARLES WASONGA June 5th, 2025 Kusoma ni dakika: 1

SERIKALI ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) imeamuru vyombo vya habari nchini humo kutoripoti shughuli za Rais wa zamani Joseph Kabila wala kufanya mahojiano na wafuasi wa chama cha kiongozi huyo.

Marufuku hiyo inajiri baada ya Kabila kurejea nchini DRC mwezi jana huku uhasama kati ya na serikali ya mrithi wake Rais Felix Tshisekedi ukikithiri.

Serikali inapanga kumfungulia mashtaka Bw Kabila kwa tuhuma za uhaini kwa misingi ya madai kuwa anashirikiana na waasi wa M23 wanaopigana na jeshi la DRC. Hata hivyo, Kabisa amewahi kukana madai hayo.

Shirika lolote la habari ambalo litakiuka marufuku hiyo itapokonywa leseni ya kuhudumu, akasema mkuu wa Baraza Kuu la Kusimamia Vyombo vya Habari (CSAC), nchini DRC Christian Bosembe.

Ikijibu tangazo la baraza hilo, msemaji wa M23, alisema vyombo vya habari katika sehemu kadhaa nchini humo viko chini ya udhibiti wake na havitazingatia marufuku hiyo.

Bw Kabila hakutoa kauli yoyote kuhusu hatua hiyo ya serikali ya DRC, lakini Katibu wa chama cha Kabila, “People’s Party for Reconstruction and Democracy (PPRD)” Ferdinand Kambere alipuuzilia mbali marufuku hiyo akisema  ilitolewa “kiholela”.

Wiki jana, Kabila alionekana katika mjini wa Goma, uliooko mashariki mwa DRC, na unaodhibitiwa na waasi wa M23.

Amekuwa akiikosoa vikali serikali baada ya Seneti kuondoa kinga aliyopewa dhidi ya kushtakiwa kwa “kosa” hilo hilo la kuunga mkono M23.

Taifa jirani la Rwanda pia limelaumiwa kwa kuunga mkono kundi hilo la waasi, lakini limekataa.

Bw Kabila, ambaye hajafunguliwa mashtaka kwa kosa lolote, mwezi jana aliikashifu serikali ya DRC, akiitaja kama ya “kidikteta”.