Kimataifa

Kamala Harris aahidi kuhalalisha bangi akishinda urais Amerika

Na MASHIRIKA October 16th, 2024 Kusoma ni dakika: 2

DETROIT, AMERIKA

MGOMBEA urais wa Chama cha Democratic nchini Amerika, Kamala Harris, jana aliahidi kuhalalisha bangi na kushinikiza mageuzi katika sekta hiyo huku akiendelea kutafuta uungwaji mkono kutoka kwa wanaume weusi nchini humo.

Harris alisema hayo jana katika mahojiano na mtangazaji wa redio Charlamagne tha God.

Charlamagne, mcheshi na mwandishi wa habari ambaye huandaa kipindi cha redio “The Breakfast Club”, anajulikana kwa mahojiano yake yanayolenga watu mashuhuri nchini humo.

Ingawa yeye ni mfuasi wa Harris, amekuwa akimkosoa na Rais Joe Biden siku za nyuma na kuwarejelea kama watu “waoga” kwa kutoendesha kesi dhidi ya mgombea urais wa Republican, Donald Trump.

Katika mojawapo ya maswali yake ya kwanza, mwandishi huyo wa habari alimtaka Harris azungumzie uvumi kwamba aliwafungia wanaume Weusi kwa zaidi ya miaka kumi na miwili kama wakili wa Wilaya ya San Francisco.

“Si kweli,” Harris alisema, akiongeza kuwa alikuwa kama mmoja wa waendesha mashtaka kwenye kesi za bangi.

Alisema kama rais, atafanya kazi ya kuhalalisha bangi kwa sababu alijua jinsi sheria zimefinya watu fulani, haswa wanaume Weusi.

Haya yanajiri huku kura nyingine za maoni zikionyesha kuwa wanaume Weusi wachache tu ndio wanamuunga mkono Harris ikilinganishwa na wakati wa kampeni za Biden katika uchaguzi wa 2020.

Kampeni yake na washirika wake akiwemo Barack Obama wanajitahidi kuvutia tena Michigan na majimbo mengine.

Harris alisema moja ya changamoto kubwa anazokabiliana nazo ni habari potofu kutoka kwa timu ya Trump inayolenga wapiga kura Weusi.

“Wanajaribu kuwatishia watu kwa sababu wanajua vinginevyo hawana chochote cha kukimbilia,” alisema.

Alipoulizwa kuhusu jinsi angezuia ukatili wa polisi na mauaji ya wanaume Weusi, Harris alisema atafanya kazi kupitisha Sheria ya George Floyd, ambayo ilikwama katika Bunge la Congress mnamo 2021.

Charlamagne alijibu kwamba labda Harris hakuweza kupata kura, rejeleo la Bunge la Amerika lililogawanyika vikali na akauliza kwa nini anapaswa kushinikiza hilo.

“Sikubaliani na mbinu hiyo,” Harris alisema, akiongeza kuwa alitekeleza wajibu kadhaa ikiwemo kupitisha haki za kupiga kura.

Hata hivyo, alikataa kujibu moja kwa moja ikiwa alifikiri Mwanasheria Mkuu, Merrick Garland, alipaswa kumweka Trump gerezani kwa kushambulia Ikulu ya Amerika mnamo Januari 6, 2021.

“Nadhani mahakama inapaswa kushughulikia hilo,” alisema.

“Nitashughulikia Novemba,” akaongezea.

Waliopiga simu wakati wa mahojiano hata hivyo walisema wanahofia kwamba uchaguzi nchini humo huenda usiwe huru na wa haki au kwamba Trump atajaribu kuleta ghasia mnamo Januari 6.

Hata hivyo, Harris hakujibu hayo ila akasema, “Mwanaume huyu ni dhaifu na hafai kabisa urais.”

Pia aliorodhesha mapendekezo yake ya kiuchumi yaliyowalenga watu Weusi, na sera nyingine zinazolenga wamiliki wa biashara ndogo ndogo na kupunguza bei ya dawa za kulevya.