Kimataifa

Musk akubali kusitisha cheche dhidi ya Trump

Na REUTERS June 6th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

BILIONEA na mmliki wa mtandao wa X Elon Musk Ijumaa aliashiria kuwa angepunguza cheche kali kati yake na Rais wa Amerika Donald Trump baada ya wawili hao kukabiliana vikali hadharani mnamo Alhamisi usiku.

Musk ambaye ni Afisa Mkuu Mtendaji wa Kampuni ya Tesla alisema kuwa huenda angelemaza utendakazi wa ndege za kusafirisha mizigo angani za Amerika ambazo ziliundwa na kampuni yake na zimekuwa zikitumiwa na serikali.

Bwanyenye huyo anasemakana alipunguza hasira zake dhidi ya Trump baada ya kutakiwa afanye hivyo na bilionea mwenzake Bill Ackman ambaye alimtaka azike tofauti zake na kiongozi huyo wa Amerika.

Katika hatua ambayo ilionekana kama kuingiwa na uoga, Ikulu ya White House pia baadaye Ijumaa ilikuwa imepanga mazungumzo kati ya Trump na Musk ili kutuliza hali na kuepusha cheche kali zaidi.

Wakipapurana, Trump alionyesha kukerwa kwake na Musk kukosoa sera yake ya ushuru na mswada wa matumizi ya serikali. Musk pia alisema sera za kibiashara za Trump zitasababisha kuporomoka zaidi kwa uchumi wa Amerika na akapendekeza atimuliwe madarakani.

Musk hakukomea hapo cheche hizo zilipokuwa zikiendelea kwa kuwa alimhusisha Trump na kuwa na uhusiano na Jeffrey Epestein, raia wa Amerika anayetumikia kifungo kutokana na dhuluma ya ngono dhidi ya watoto.

Trump naye alikuwa ametishia kuwa Amerika ingefuta kandarasi zake zote ila Musk akamjibu kuwa angeporomosha jukwaa la mtandao la usafirishaji mizigo angani, Dragon spacecraft ambalo pia hutumiwa na NASA.

Ijumaa, Musk akimjibu mmoja wa watumiaji wa X alisema kuwa asingeporomosha mtandao huo huku jamaa huyo akimtaka yeye na Trump wasitishe uhasama.

“Hujakosea,” Musk akajibu chapisho la bilionea mwenzake Ackman ambaye alimtaka pamoja na Trump waridhiane kwa ajili ya umoja wa Amerika.

Duru zinaarifu kuwa wandani wa Trump nao walimbembeleza akomeshe cheche kali za hadharani dhidi ya Musk na wakamshawishi akubali kuzungumza naye kwa simu kama ishara ya maridhiano.

Licha ya kukubali maridhiano, Trump anasema cheche hizo zilimwongezea umaarufu zaidi kisiasa na miongoni mwa raia wa Amerika.
“Nimefanya vizuri na hata takwimu zinaonyesha umaarufu wangu umepanda hata kuliko wa hapo awali,” akasema Trump.

Pia wandani wa Trump walimshauri amakinikie kushawishi Seneti ipitishe mswada wa ushuru na matumizi ya serikali badala ya kutifuana na Musk.

“Sina tatizo hata kama Elon amenigeuka lakini angefanya hivyo miezi kadhaa iliyopita. Mswada wa ushuru ni kati ya miswada bora zaidi ambayo imewahi kupitishwa na Bunge la Congress,” akaongeza Trump.