Trump aipa Iran siku 10 zaidi kufungua Mkondo wa Hormuz vita vikichacha
RAIS wa Amerika, Donald Trump, ametangaza kuongeza muda wa siku 10 kwa Iran kufungua tena Mkondo wa Hormuz, akionya kuwa isipofanya hivyo basi itashambulia mitambo yake ya nishati.
Hatua hiyo imejiri huku mvutano wa kijeshi kati ya Iran, Amerika na Israeli ukizidi kuongezeka, hali ambayo tayari imesababisha vifo vya maelfu ya watu na kuyumbisha uchumi wa dunia.
Kupitia ujumbe kwenye mtandao wa Truth Social, Trump alisema mashambulizi yaliyokuwa yamepangwa dhidi ya miundombinu ya nishati ya Iran yamesitishwa hadi Aprili 6 akidai kuwa uamuzi huo ulifuatia ombi kutoka Iran.
“Hata hivyo mazungumzo yanaendelea vizuri licha ya taarifa potofu,” alisema Trump.
Iran imekanusha vikali madai ya kuwa katika mazungumzo ya moja kwa moja na Amerika huku viongozi wake wakisisitiza kuwa hawajakubali masharti yaliyowasilishwa kupitia mpango wa vipengele 15 uliopitishwa na Pakistan.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Ujerumani, Johann Wadephul, alifichua kuwa kuna mawasiliano ya siri kati ya pande hizo mbili na kwamba mkutano wa ana kwa ana unaweza kufanyika hivi karibuni nchini Pakistan.
Wakati huo huo, Iran imezidi kuimarisha msimamo wake kwa kufunga Mkondo wa Hormuz, njia muhimu inayopitisha karibu asilimia 20 ya mafuta na gesi ya dunia.
Hatua hiyo imechangia kupanda kwa bei ya mafuta ghafi duniani.
Mashambulizi ya anga pia yameripotiwa kuendelea nchini Iran, huku watu sita wakithibitishwa kufariki katika eneo la Qom baada ya majengo kushambuliwa.
Katika mji wa Urumia, kombora lililorushwa katika jengo la makazi lilisababisha vifo na majeruhi kadhaa.
Jeshi la Israeli limesema lilishambulia kituo kikuu cha Iran cha kutengeneza makombora na mabomu ya baharini katika mji wa Yazd.
Ndani ya Iran, mamlaka zimeripoti kukamatwa kwa watu wanaodaiwa kushirikiana na shirika la ujasusi la Israeli, Mossad, wakipanga mashambulizi dhidi ya maeneo nyeti ya kijeshi.
Athari za vita hivi zimeanza kuonekana kimataifa, huku bei ya mbolea na nishati ikipanda kwa kasi na kuzua hofu ya mfumuko wa bei.
Huku baadhi ya washirika wa Amerika wakisita kushiriki katika operesheni ya kufungua Mkondo wa Hormuz, juhudi za kidiplomasia zinaonekana kukumbwa na changamoto kubwa.
Hata hivyo, afisa mmoja wa Iran alinukuliwa akisema kuwa licha ya kukataa pendekezo la Amerika, milango ya mazungumzo bado haijafungwa kabisa.