Trump atishia kurejelea kuilipua Iran isipokubali mpango wake wa amani
WASHINGTON, Amerika:
RAIS Donald Trump ameitaka Iran izinduke haraka na itie saini mkataba wa makubaliano la sivyo ijiandae kushambuliwa na pia Amerika itaendelea kuzuia uchukuzi wa majini wa meli zake.
Trump alielezea kusikitishwa na mkondo wa mazungumzo ya amani kati ya Amerika na Iran huku akionya kuwa Iran lazima iharakishe kutia saini makubaliano ya kupatikana kwa amani ya kudumu.
Kupitia mtandao wake wa Truth Social, Trump amesisitiza kuwa Iran haifai kuruhusiwa kumiliki zana za kinyuklia na ni dhahiri taifa hilo limeshindwa kujipanga huku subira yake nayo ikiendelea kuisha.
Maafisa wa Amerika walifichua kuwa wameagizwa waendelee kuzuia Iran kutumia bandari ndipo taifa hilo likubali matakwa ya Amerika.
Trump hasa analenga kudhoofisha uchumi wa Iran ili kulazimisha taifa hilo kujisalimisha na kutii masharti yake kabla ya kumaliza vita.
“Hawajui jinsi ya kutia saini makubaliano yasiyo ya nyuklia. Ni afadhali wawe makini haraka,” akasema Trump bila kufafanua makubaliano hayo yangekuwa na masharti gani.
Iran inataka Amerika itambue haki yake ya kutengeneza na kustawisha viwanda vyake vya nyuklia ikisema ni kwa matumzi ya nyumbani.
Nchi hiyo imekanusha kuwa inatengeneza nyuklia kwa ajili ya kivita.
Maafisa wa Iran walisema Jumanne kuwa nchi hiyo inaweza kustahimili uchumi wake licha ya kuzuiwa kutumia bandari yake.
Walisema wana njia mbadala za biashara, na kwamba bado wanajiandaa kwa vita wakati wowote dhidi ya Amerika.
Vita kati ya Amerika-Israel dhidi ya Iran, vimesababisha mauaji ya maelfu ya watu Ukanda wa Mashariki ya Kati huku wengine wakilazimishwa kuhama makwao.
Pendekezo la hivi karibuni la Iran la kumaliza vita hivyo vya miezi miwili vilivyositishwa tangu Aprili 8 chini ya makubaliano, linataka mjadala kuhusu mpango wake wa nyuklia uahirishwe hadi mzozo utakapomalizika rasmi na matatizo ya usafirishaji baharini kutatuliwa.
Hata hivyo, pendekezo hilo halikukidhi sharti la Trump la kuanza kujadili suala la nyuklia tangu mwanzo.
Matumaini ya suluhu ya haraka yamepungua baada ya Trump mwishoni mwa wiki iliyopita kufuta ziara ya mjumbe wake maalum Steve Witkoff pamoja na mkwewe Jared Kushner kuenda Pakistan kwa mazungumzo ya upatanishi.
Waziri wa mambo ya nje wa Iran, Abbas Araqchi, alitembelea nchi hiyo mara mbili mwishoni mwa wiki jana.
Baada ya viongozi kadhaa wa kisiasa na kijeshi wa Iran kuuawa katika mashambulizi ya Amerika na Israel, Iran inaonekana haina tena kiongozi mmoja mwenye mamlaka ya juu ambaye anaweza kutoa mwelekeo wakati wa mazungumzo