Kimataifa

Watu 20 wafariki Tanzania kufuatia maporomoko ya ardhi

Na MASHIRIKA, WINNIE ONYANDO March 27th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

WATU wasiopungua 20 wamefariki kusini mwa Tanzania katika mkoa wa Mbeya, kufuatia maporomoko ya ardhi yaliyosababishwa na mvua kubwa ilioambatana na upepo mkali.
Mkuu wa wilaya ya Rungwe, Jaffar Haniu ambako maafa hayo yalitokea siku ya Jumatano, amesema maporomoko hayo pia yaliharibu nyumba kadhaa, huku idadi ya vifo ikihofiwa kuongezeka.
Kulingana na ripoti ya Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mbeya, Benjamin Kuzaga, janga hilo lilifikia maeneo ya Nkunga, Lupepo, Kawetele, na Ikuti.
Waathiriwa walikuwa watu wazima wanne na watoto 14, wakiwamo wasichana wanane na wavulana sita.
Miongoni mwa waathiriwa walikuwa Chapakazi Mwasota, 60, Lida Mwangimwa, 55, Neema Mwasema, 31, na Annet Morohani, 35.
Watoto waliopoteza maisha yao ni pamoja na watoto wachanga wenye umri wa miezi 10.
Watu wengine watano walipata majeraha mbalimbali na sasa wanapokea matibabu katika Hospitali ya Wilaya ya Makandana huko Tukuyu na Zahanati ya Chuo cha Magereza cha Kiwira.
Mamlaka ya hali ya hewa nchini Tanzania imetabiri mvua kubwa katika sehemu nyingi za nchi hiyo hadi Jumanne wiki ijayo.
Eneo la Afrika Mashariki limekumbwa kwa wiki kadhaa sasa na mvua kubwa ambazo mwezi huu zimesababisha vifo vya watu 81 na kuwaacha maelfu bila makazi.