Kivumbi Gachagua na Murkomen wakivurugana kwa maneno makali: ‘Umelewa madaraka’
JOTO la kisiasa nchini limezidi kupanda huku viongozi wa upinzani wakimjia juu Waziri wa Usalama Kipchumba Murkomen, kufuatia msururu wa mashambulizi ya maneno dhidi ya kiongozi wa chama cha DCP, Rigathi Gachagua.
Wakizungumza jana wakati wa ibada katika Kanisa la AIC Namanga, Kajiado, viongozi wa Muungano wa Upinzani wakiongozwa na kinara wa Wiper Kalonzo Musyoka, Justin Muturi (DP) na Eugene Wamalwa (DAP-K), walimkashifu Murkomen kwa kile walichokitaja kama “ulevi wa madaraka” na kukosa nidhamu ya kiofisi.
Mvutano huo umejitokeza huku kumbukumbu za maandamano ya Juni 25, 2024 zikiendelea kutawala anga ya kisiasa na kuibua maswali kuhusu usalama na mwelekeo wa nchi.
Akimtetea Bw Gachagua dhidi ya makombora ya Bw Murkomen, kiongozi wa chama cha DP Justin Muturi amemtaja waziri wa usalama kama kiongozi aliyetekwa na mamlaka.
“Ulipewa cheo kikubwa lakini ofisi imekuingia kichwani ukawa mlevi wa madaraka,” akasema Bw Muturi.
Naye Kalonzo Musyoka aliongeza kuwa cheche za waziri huyo si zake binafsi bali ni msimamo wa Ikulu, huku akisisitiza kuwa upinzani hautaruhusu mgawanyiko wowote wa kisiasa kwa misingi ya vitisho.
“Matamshi ya Bwana Murkomen ni matamshi ya Bwana Ruto. Hapa Kenya haiwezekani kutisha wananchi na pia kutisha vyombo vya habari. Hilo ni jaribio lisilowezekana kabisa na la kipumbavu mno,” akafoka Bw Kalonzo.
Malumbano hayo yamechochewa na matamshi makali aliyotoa Jumamosi, Bw Murkomen akiwa Moiben, Uasin Gishu, ambapo alimdunisha Bw Gachagua na kikosi kizima cha upinzani akidai hawana uwezo wowote wa kutikisa serikali ama kumshinda Rais William Ruto katika uchaguzi mkuu ujao.
“Hata hawezi kuwa mtu wa kusimamia kamati ya kujenga choo kijijini. Hawezi kwa sababu kikatiba hawezi kuwania wadhifa wa umma asimamie mtu yeyote,” alidai Bw Murkomen.
Kama kwamba hiyo haitoshi, akihudhuria ibada ya kanisa la AIC Kamuneru, Mt Elgon, Bungoma jana, Murkomen aliongeza makombora mengine mapya akisisitiza kuwa serikali haitayumba.
“Sisi katika sekta ya usalama tumeweka mikakati ya kutosha kuhakikisha kwamba watu wa sampuli yake hawapati nafasi ya kutuharibia taifa letu. Nilikuwa ninaona jana anasema atasimamisha nchi; anasimamisha nchi kama yeye ni nani? Mtu alifukuzwa kazi hata hakumaliza nusu mwaka hawezi, hana uwezo huo. Nchi hii iko thabiti katika uongozi wa Rais William Ruto,” alirusha cheche Bw Murkomen.
Mbali na vita hivyo vya maneno, upinzani pia ulimlenga Rais William Ruto kufuatia malumbano yake ya hivi punde na kinara wa chama cha KANU Gideon Moi kuhusiana na hatua ya serikali ‘kuminya uhuru wa vyombo vya habari.’
Huku hayo yakijiri, vinara hao wa upinzani wametangaza mikakati ya kuongoza maadhimisho mengine Julai 7 (Saba Saba), wakishikilia kuwa wanataka haki itendeke kwa waathiriwa wa ukiukaji wa haki za kibinadamu zaidi ya mchakato wa fidia unaoshinikizwa na serikali kwa sasa.