BITUGI MATUNDURA: ‘Mdomo tamu tamu’ uliomjenga Ruto kisiasa 2022 utamfaa 2027?
KAMPENI za kinyang’anyiro cha urais 2022 zilipokuwa kileleni, aliyekuwa rais, Bw Uhuru Kenyatta aliwatahadharisha Wakenya mara kadhaa wajiepushe kuwachagua viongozi wenye “mdomo tamu tamu.”
Nadhani Rais Uhuru Kenyatta alikuwa akimrejelea naibu wake, Dkt William Ruto, aliyekuwa mpinzani mkuu wa Bw Raila Odinga (marehemu).
Bw Kenyatta alikuwa anamuunga mkono katika kipute hicho ili awe rais wa tano.
Uhuru alionya umma kwamba ‘maneno matamu lakini matupu” aghalabu hutumiwa kuwafumba macho na huishia kuwa ahadi tupu.
“Hawa watu wa mdomo tamu tamu watakuja hapa na maneno mengi na ahadi tupu, lakini hawana chochote cha kuwapatia,” akaonya Bw Kenyatta.
Aidha Bw Kenyatta alikuwa akirejelea ‘masimulizi ya Hasla’ (Hustler narrative) ambayo yalitumiwa na mrengo wa siasa wa Kenya Kwanza kama kaulimbiu ya kuwashawishi wapigakura.
Dkt Ruto hatimaye aliibuka mshindi kwenye uchaguzi Mkuu wa 2022 kwa kuzoa kura 7,176,141 (50.49%) katika chama cha United Democratic Alliance (UDA) naye Bw Odinga wa Orange Democratic Movement (ODM) akapata kura 6,942,930 (48.85%).
Ushindi wa Ruto yamkini uliwashangaza wengi walioamini kwamba Bw Odinga angembwaga kwa misingi kwamba mamlaka ya dola fiche (deep state) yangempiga jeki Odinga.
Tukio hilo mpaka sasa limewashangaza wengi. Hata hivyo, ushindi wa Ruto katika uchaguzi mkuu wa 2022 hauhitaji maarifa ya sayansi ya roketi kuelezea.
Kwanza, Ruto alikuwa na mikakati mizuri. Pili, ‘mdomo tamu tamu’ ulishawishi jamii ya Agikuyu yenye wingi wa kura.
Jamii ya Agikuyu pekee ilimpigia Bw Ruto asilimia 77 ya kura za eneo la Mlima Kenya, huku Bw Odinga akizoa asilimia 22 pekee ya kura za eneo hilo.
Mbali na kuwa mlumbi mzuri, sera alizonadi Rais Ruto kuhusu mikakati ya kuwainua wanyonge (mahasla) ziliwashawishi watu wengi, zikiwemo asasi za kidini.
Miaka mitatu ya uongozi wa Rais Ruto inaelekea kuwakatisha tamaa wanachi waliokuwa na matumaini makubwa.
Serikali ya UDA inaonekana ‘kusema sana’ kuliko inavyotenda. Ahadi nyingi zilizokuwa kwenye rajua au Manifesto ya Rais Ruto hazijatekelezwa mpaka sasa.
Gharama ya maisha imepanda. Uchumi umedorora na kusababisha kampuni nyingi kuhamia nchi jirani kwa sababu ya gharama kubwa ya kuziendesha.
Ufisadi umekithiri huku mifumo ya ufadhili wa elimu na Afya (matibabu) ikiyumbayumba kila uchao.
Kutokana na hali hii, inabainika bayana ubashiri wa Bw Uhuru Kenyatta kuhusu hatima ya Kenya chini ya uongozi wa Ruto unatimia.
Hali hii inatuchochochea kuuliza swali alilouliza mshairi – Abdilatif Abdalla: Kenya: Twendapi?
Bitugi Matundura ni mhadhiri, Chuo Kikuu cha Chuka
mwagechure@gmail.com