Habari

Korti yazuia madiwani kumtimua afisa wa Kaunti

Na CYNTHIA MAKENA Na NICHOLAS NJOROGE June 28th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

MAHAKAMA Kuu imesitisha mipango ya madiwani wa Kaunti ya Nairobi kumwondoa mamlakani afisa mkuu wa makazi, Bi Lydia Mathia.

Jaji Bahati Mwamuye alitoa amri inayowazuia madiwani dhidi ya kumbandua Bi Mathia afisini hadi kesi aliyowasilisha isikizwe na kuamuliwa.
Mahakama imezuia Bunge la Kaunti kutekeleza uamuzi ambao ulipitishwa mnamo Juni 24 au kuchukua hatua zozote zile dhidi ya afisa huyo.
Jaji huyo kisha aliamrisha Bi Mathia akabidhi madiwani na serikali ya kaunti amri hiyo ya korti.
“Mahakama inatoa amri inayozuia kuondolewa kwa Bi Mathia afisini hadi kusikizwa na kuamuliwa kwa kesi aliyoiwasilisha,” akasema Jaji Mwamuye. Kesi hiyo itatajwa mnamo Agosti 11 ambapo mwelekeo utatolewa kuhusu siku ambayo itasikizwa.
Kwenye kesi hiyo Bi Mathia alisema uamuzi wa madiwani ulikuwa haramu na haukufuata katiba. “Hoja hiyo ilikuwa haramu kwa sababu hakukuwa na ombi kwa bunge kuniondoa afisini. Badala yake walitoa mapendekeo na uamuzi wa kufanya uchunguzi ambao ulibainika baadaye ulikuwa wa kunitimua,” akasema Bi Mathia.
Afisa huyo wa kaunti amekashifiwa kwa matumizi mabaya ya afisi, ukiukaji wa haki za raia, kupuuza amri ya korti kuhusiana na kutimuliwa kwa wapangaji kwenye nyumba za kaunti.
Madiwani walimtimua baada ya umma kulalamika kuhusu kuondolewa kwa lazima kwenye nyumba za kaunti katika mitaa ya Old Ngara, New Ngara, Kariokor, Buruburu, Kariobangi na Woodley.
Kupitia wakili Moses Mabeya, Bi Mathia alisema uamuzi wa kuondolewa afisini ulikuwa haramu kwa sababu hakupewa nafasi ya kusikizwa.
“Mteja wangu alisulubishwa bila kusikizwa na hii inakiuka sheria ambapo afisa wa umma anastahili kusikizwa iwapo anakabiliwa na madai kabla ya kuondolewa afisini,” akasema Bw Mabeya.
Wakili huyo alisema Bunge la Kaunti lilivuka mipaka na kuingilia haki za kikatiba za mteja wake.
Wakazi waliondolewa kwenye nyumba zao licha ya kuwa kesi ambayo walikuwa wamewasilisha mahakamani bado haikuwa imeamuliwa.
Madiwani pia walipendekeza kuwa Bodi ya Ajira ya Kaunti ya Nairobi ichukue hatua za kinidhamu kwa kumwondoa Bi Mathai afisini.