Habari

Murkomen asema Polisi Gen-Z watakabiliana na wahuni 2027

Na MERCY MWENDE May 9th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

SERIKALI imeweka matumaini makubwa kwa kizazi kipya cha maafisa wa polisi wa Gen-Z wanaotarajiwa kuhitimu ndani ya miezi mitatu kutoka Chuo cha Polisi cha Kitaifa cha Kiganjo, ili kusaidia kukabiliana na wahuni na changamoto nyingine za kiusalama kuelekea uchaguzi wa 2027.
Haya yanajiri huku ikifichuka kuwa makurutu 54 wamefurushwa kutoka mafunzo yaliyoanza Septemba mwaka jana, ambapo 18 walitimuliwakwa sababu ya ujauzito.
Waziri wa Usalama wa Ndani Kipchumba Murkomen alisema ana imani kuwa maafisa hao vijana wataweza kukabiliana na ongezeko la makundi ya wahuni wanaodaiwa kufadhiliwa na wanasiasa.
“Nataka mjue tumekuwa tukiwaombea.Kwa nguvu mlizo nazo, sidhani wahuni wetu wataweza kuhimili,” alisema.
Chuo hicho kilithibitisha kuwa jumla ya makurutu 54 wameondolewa katika mafunzo hayo.
Kati yao, 18 waligundulika kuwa wajawazito, wengine 18 walitumia vyeti bandia, wawili walitumia vitambulisho vya kughushi, wawili walikuwa na matatizo ya kiafya, watatu walikuwa na makosa ya nidhamu, 10 walikuwa na rekodi za uhalifu wa awali, na mmoja aliachana na mafunzo kwa sababu za ugonjwa.
Kwa sasa chuo hicho kina zaidi ya makurutu 4,000.
Akizungumza wakati wa zoezi la tathmini katika chuo cha makurutu wa polisi cha Kiganjo Alhamisi, Murkomen ambaye aliandamana na Inspekta Jenerali Douglas Kanja na Naibu Inspekta Jenerali Eliud Lagat, alitangaza mpango wa kukiboresha chuo hicho na kukifanya chuo kikuu kamili cha polisi.
Alisema chuo hicho kipya kitakuwa kituo cha kikanda cha mafunzo kwa maafisa kutoka Afrika na mataifa mengine kupitia ushirikiano wa kimataifa.