Maoni

MAONI: Walimu waonyeshe mfano wa nidhamu hata wanapotumia mitandao ya kijamii

Na BENSON MATHEKA August 18th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KANUNI za kuimarisha nidhamu miongoni mwa walimu ni hatua inayofaa, hasa katika enzi hii ambapo mitandao ya kijamii imekuwa sehemu muhimu ya maisha ya kila siku.

Mwalimu si mfanyakazi wa kawaida. Yeye ni mlezi, mshauri na kioo cha jamii.

Kwa hivyo, mwenendo wake shuleni na nje ya shule unaweza kuwa na athari kubwa kwa wanafunzi na jamii kwa ujumla.

Mitandao ya kijamii imeleta fursa kubwa za mawasiliano, kujifunza na kubadilishana mawazo. Lakini pia inaweza kuwa chanzo cha mienendo inayodhalilisha hadhi ya mwalimu.

Lugha chafu, matusi, picha zisizofaa, ulevi wa kujionyesha hadharani na matusi dhidi ya watu wengine vinaweza kumfanya mwalimu apoteze heshima anayopaswa kuwa nayo mbele ya wanafunzi na wazazi.

Mwalimu anayewafundisha wanafunzi kuhusu heshima, nidhamu na uwajibikaji hawezi kuhubiri maadili hayo darasani halafu akafanya kinyume chake kwenye mitandao.

Hata hivyo, kanuni hizo hazipaswi kutumiwa kuwanyamazisha walimu au kuwanyima haki yao ya kutoa maoni.

Mwalimu ni raia mwenye haki ya kujieleza. Kinachohitajika ni mipaka ya wazi kati ya uhuru wa kujieleza na tabia inayokiuka maadili ya taaluma.

Walimu pia wanapaswa kuelewa kwamba kile wanachoweka mtandaoni kinaweza kubaki huko kwa muda mrefu.

Chapisho moja la hasira au picha isiyofaa linaweza kusambaa kwa maelfu ya watu ndani ya dakika chache na hatimaye kuathiri heshima ya mwalimu, shule na hata taaluma nzima.

Kwa upande mwingine, mamlaka zinazowasimamia walimu zinapaswa kuhakikisha kanuni hizo zinatumika kwa haki. Nidhamu haimaanishi adhabu kali pekee.

Walimu wanahitaji pia kuelimishwa kuhusu matumizi salama na yenye uwajibikaji ya mitandao ya kijamii.

Ni muhimu kuwe na mafunzo ya mara kwa mara kuhusu maadili ya taaluma katika mazingira ya kidijitali.

Walimu wafundishwe namna ya kulinda faragha yao, wanafunzi na taasisi wanazofanyia kazi.

Hatua hiyo ni muhimu kwa sababu jamii inawatazama walimu kama vielelezo.

Watoto hujifunza si kutokana na vitabu na masomo pekee, bali pia kutokana na tabia za watu wanaowaongoza.

Mwalimu ni kioo cha jamii. Kioo hicho kinapaswa kuonyesha maadili tunayotarajia watoto wetu kuiga.