Mkuu wa Alliance High athibitisha stoo ilichomwa usiku, ataka wazazi wakachukue watoto wao
MWALIMU mkuu wa Shule ya Upili ya Alliance amethibitisha kwamba stoo ya magodoro ilichomwa usiku wa kuamkia Alhamisi ingawa hakuna mwanafunzi yeyote aliyejeruhiwa.
Katika ujumbe kwa wazazi Alhamisi asubuhi, mwalimu huyo aliwaita wazazi kwa mkutano wa dharura shuleni ambao ulifaa kuanza saa nne asubuhi.
Malengo ya mkutano huo, alisema, ni kujulisha wazazi kuhusu kilichojiri na hatua zilizochukulia, kuzungumzia masuala yanayozua wasiwasi, kupata mwelekeo kamili kuhusu siku zijazo na kujadili jinsi jamii ya shule inavyoweza kushirikiana.
Habari za kuzuka kwa moto zilichipuka Jumatano usiku huku video zikisambazwa kuhusu moto huo. Vyanzo vya mwanzo vilikuwa vimedai kwamba moto huo ulikuwa umetokea katika mojawapo ya mabweni ingawa baadaye ripoti zilionyesha kwamba ulikuwa katika stoo ya magodoro ya wanafunzi waliomaliza shule.
Haya yanajiri huku hofu ikigubika shule nyingi kuhusu utovu wa nidhamu, uharibifu na hata maafa.
Ni juma moja tu baada ya mkasa wa kusikitisha ambapo wanafunzi 16 walipoteza maisha yao shuleni Utumishi Girls, Gilgil baada ya kile kinachoshukiwa kuwa wenzao kutia moto bweni usiku.
Kesi hiyo ingali inaendelea kortini Naivasha.