Habari

Mvutano wazuka kuhusu usajili wa Linda Mwananchi

Na JUSTUS OCHIENG August 5th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MVUTANO kuhusu usajili wa chama kipya cha kisiasa cha Linda Mwananchi Party umechukua mwelekeo mpya baada ya mawakili wa Charles Wanyonyi, aliyekuwa wa kwanza kujaribu kukisajili kushtumu Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Kisiasa (ORPP) kwa kutaka kupitia upya uamuzi wa awali bila kumshirikisha muombaji wa kwanza.

Hatua hiyo imejiri siku moja baada ya Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna na viongozi wanaohusishwa na vuguvugu la Linda Mwananchi kukutana kwa faragha na Msajili wa Vyama vya Kisiasa John Cox Lorionokou.

Baada ya mkutano huo, viongozi hao walitangaza kuwa msajili alikubali kupitia upya uamuzi wa kukataa kuhifadhi jina la chama hicho.

Hata hivyo, mawakili wa Bw Wanyonyi wanasema hatua hiyo ni kinyume cha Katiba na haki ya kila mtu kusikilizwa iwapo mteja wao hatahusishwa katika mchakato huo.

Katika barua iliyowasilishwa kwa msajili Agosti 5, mawakili wa kampuni ya Wanzau, Odhiambo and Associates walisema Bw Wanyonyi ndiye aliyekuwa wa kwanza kuomba kuhifadhi jina la “Linda Mwananchi Party of Kenya” mnamo Februari 24, 2026.

Kwa mujibu wa mawakili hao, maombi ya kuhifadhi majina ya vyama yanapaswa kushughulikiwa kwa kufuata utaratibu wa aliyewasilisha kwanza.