Habari

Nyakango aonya serikali kuhusu kuwa kibaraka wa IMF

Na DAVID MWERE February 15th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MDHIBITI wa Bajeti, Margaret Nyakang’o ametaka serikali kutanua vyanzo vyake vya kufadhili bajeti ya taifa, akionya kwamba kutegemea mno Shirika la Kimataifa la Fedha (IMF) kunaweza kudhoofisha mageuzi ya sera ufadhili unapokatika.
Dkt Nyakang’o alimulika ukuruba wa serikali na taasisi hiyo huku pia akieleza wasiwasi wake kuhusu kuanzishwa kwa Hazina ya Kitaifa ya Miundombinu (NIF) chini ya Sheria ya Mashirika ya Serikali yanayomilikiwa na Umma.
Sheria hiyo – inayotaka mashirika ya serikali kuendeshwa kama taasisi za kibiashara kwa faida, kujifadhili na kujitegemea – ilikuwa sehemu ya masharti ya mageuzi yaliyoidhinishwa na IMF chini ya mpango wa kufadhili mashirika ya umma.
Dkt Nyakang’o anasema mipango ya IMF huambatana na makubaliano yenye gharama, “hasa masharti yanayohitaji kubana matumizi ya fedha za umma kwa haraka.”
“Hatuwezi kuwa vibaraka tu; tunahitaji kutazama suala hili kwa uhalisia,” alisema Mdhibiti huyo wa Bajeti.
Aliongeza kuwa, “Sheria hii kama tunavyoona, inapita bila uchunguzi wa Bunge wala ofisi yangu, na hivyo kudhoofisha uwajibikaji wa umma.”
Sheria hiyo ni mageuzi ya kimuundo ya kutimiza masharti ya IMF, ambapo mashirika yaliyo chini yake hufanya kazi kama kampuni chini ya Sheria ya Kampuni badala ya kuundwa kwa sheria mahsusi za Bunge.
Mfumo huu unalenga kupunguza urasimu wa serikali na mzunguko wa bajeti wa kila mwaka ili kutoa mtaji kwa miradi ya muda mrefu.
IMF imekuwa ikisisitiza mageuzi ya kimuundo ili kupunguza mzigo wa kifedha unaotokana na mashirika ya umma yanayopata hasara, na hivyo hii inalenga kufanikisha azma hiyo.
Kupitishwa kwa sheria hiyo kulikuwa ishara muhimu kwa IMF wakati Kenya ilipokuwa ikijadiliana kuhusu mpango mpya wa ufadhili kufuatia kumalizika kwa makubaliano ya awali ya Sh464.47 bilioni mapema mwaka 2025.
Hata hivyo, utekelezaji wake ulianza Februari 2, 2026, kisha kusimamishwa hadi Februari 23, 2026, baada ya Mahakama Kuu kutoa amri ya muda kufuatia kesi iliyowasilishwa na Consumers Federation of Kenya (Cofek).
Kwa mujibu wa Dkt Nyakang’o, huku Kenya ikiingia katika mpango mpya wa IMF, ni lazima ishughulikie mapengo ya uaminifu na utekelezaji ambayo, anasema, yanazuia matumizi ya kijamii, kubana maendeleo na kuchochea upinzani wa kisiasa maisha yanapokuwa magumu kwa wananchi.
“Tunahitaji kuangalia sera za kubana matumizi zinazotekelezwa mapema ambazo zinaweza kupunguza ustawi wa familia na kudhoofisha ukuaji wa uchumi,” alisema.