ODM yasisitiza sera zake zijumuishwe manifesto ya Ruto
CHAMA cha ODM kinataka baadhi ya sera zake muhimu zijumuishwe katika manifesto ya uchaguzi ya Rais William Ruto ya 2027 kama sehemu ya makubaliano ya kabla ya kuunda muungano kati ya chama hicho na UDA.
Chini ya uongozi wa Seneta wa Siaya Dkt Oburu Oginga, ODM pia inataka kuundwa kwa kikosi cha pamoja cha kiufundi kati yake na UDA ili kubaini maeneo ambapo vyama hivyo vinaweza kukubaliana kusimamisha wagombea wa pamoja au kutopambana.
Kutengwa huko kwa maeneo kumekuwa suala lenye utata, huku UDA ikipinga lakini ODM ikisema ni miongoni mwa masharti yake muhimu ili kumuunga mkono Rais Ruto katika uchaguzi wa 2027.
Mwenyekiti wa ODM Gladys Wanga alisema chama hicho kinashinikiza sera zinazohusisha ushirikishaji katika masuala ya umma, kuimarishwa kwa ugatuzi, kugawanywa kwa haki kwa rasilimali ya taifa na kuimarishwa kwa vita dhidi ya ufisadi.
Masuala mengine ni elimu bora na huduma za afya nafuu. ODM pia inaunga mkono mpango wa Nyumba za Gharama Nafuu, lakini inataka ugawaji wake uwe wa haki na uwazi.
Rais Ruto na Dkt Oburu tayari wameunda kikosi cha kiufundi cha watu 10 kuandaa manifesto ya pamoja, huku kikosi kingine kikitarajiwa kushughulikia mazungumzo ya muungano.