WALIOBOBEA: Burudi Nabwera alivuma kisiasa wakati wa Kanu
BURUDI Nabwera alikuwa miongoni mwa wanasiasa wasomi zaidi waliohitimu kutoka taasisi mashuhuri za Uingereza wakati wa ukoloni.
Elimu hiyo ilimwezesha kuelewa mifumo ya ubepari wa Magharibi na ujamaa wa Mashariki, maarifa yaliyomsaidia katika siasa na diplomasia baada ya Kenya kupata uhuru.
Baada ya uhuru, Rais wa kwanza wa Kenya, Jomo Kenyatta, alimteua kuwa balozi nchini Amerika. Chini ya Rais Daniel arap Moi, Nabwera alipanda kutoka kuwa Katibu Mkuu wa KANU hadi kuwa Waziri katika Ofisi ya Rais, moja ya nyadhifa zenye ushawishi mkubwa serikalini.
Alizaliwa mwaka 1924 na kusomea Maseno School, Chuo Kikuu cha Makerere nchini Uganda na London School of Economics.
Akiwa Maseno, alikutana na Jaramogi Oginga Odinga, ambaye baadaye alikuwa Makamu wa Kwanza wa Rais wa Kenya.
Wengine waliosoma hapo ni Masinde Muliro na Wycliffe Wasia Awori, ambao baadaye walikuwa miongoni mwa wabunge wa kwanza wa Kenya katika Baraza la Kutunga Sheria (Legco).
Akiwa Makerere, Nabwera alikutana na wasomi kama Bethwel Ogot, Thomas Odhiambo, Josephat Karanja, aliyewahi kuwa Makamu wa Rais chini ya Moi, pamoja na mshairi wa Uganda Henry Muwanga Barlow, mwandishi wa shairi maarufu Building the Nation.
Katika kitabu chake How it Happened, Nabwera alisema watu hao walimhimiza na kumsaidia kujenga taaluma yake ya baadaye.
Katika uchaguzi wa kwanza wa kitaifa baada ya enzi ya Kenyatta mwaka 1979, Nabwera alishindwa na Joshua Angatia katika kiti cha ubunge cha Lurambi North.
Wakati wa utawala wa Kenyatta, alikuwa mwanasiasa mwenye ushawishi na Waziri Msaidizi wa Mashauri ya Kigeni.
Moi alitaka kuwatumia wanasiasa wakongwe pamoja na rafiki yake Moses Mudavadi kukabiliana na siasa kali za Martin Shikuku, Lawrence Sifuna na Waziri Elijah Mwangale, ambaye rais hakumwamini.
Baada ya Mwanasheria Mkuu Charles Njonjo kuporomoka kisiasa kufuatia uchunguzi kuhusu madai ya “uhaini”, Moi alianza kupanga upya KANU.
Alimteua David Okiki Amayo kuwa mwenyekiti na Nabwera kuwa Katibu Mkuu wa tatu wa chama hicho.
Katika kipindi hicho, Nabwera alijenga sifa ya kuwa mwanasiasa mkali, akitangaza sera za chama na kutishia wanachama waliokiuka maagizo kwa hatua za kinidhamu au kutimuliwa.
Alipata umaarufu mkubwa mwaka 1986 baada ya kuonekana kwenye runinga ya taifa, Voice of Kenya (VoK), na kutangaza kwamba KANU ilikuwa tayari kuwasamehe wanasiasa waliofahamika kama “watu wa Njonjo”.
Kauli hiyo ilizua hasira ndani ya KANU kwa sababu wakati huo ilikuwa mwiko kufikiria kuwasamehe wanasiasa waliokuwa wamehusishwa na Njonjo.
Moi alikuwa amemshutumu Njonjo kwa kupanga njama na nchi ya kigeni kuangusha serikali. Rais alianzisha tume ya uchunguzi iliyoongozwa na Jaji Cecil Miller, ambayo hatimaye ilimsafisha Njonjo.
Hata hivyo, wanasiasa kadhaa waliodaiwa kuwa washirika wake walikuwa tayari wameanguka kisiasa.
Kauli ya Nabwera ilipewa uzito mkubwa na vyombo vya habari, lakini ndani ya Ikulu na miongoni mwa viongozi wakuu wa KANU haikupokelewa vyema.
Baadhi yao walimshutumu kwa kuwa mfuasi wa Njonjo. Muda mfupi baadaye, aliondolewa kama Katibu Mkuu na nafasi hiyo ikachukuliwa na Mudavadi.
Akiwa Waziri wa Nchi katika Ofisi ya Rais, Nabwera alikuwa na ushawishi mkubwa kuliko hata Katibu Mkuu wa KANU.
Ofisi yake katika Harambee House ilitembelewa na wafanyabiashara, watu waliokuwa wakitafuta ajira na mabroka wa kisiasa waliotaka apelekee ujumbe wao kwa Rais Moi.
Hata hivyo, kosa lake kubwa lilikuwa kushindwa kutofautisha masuala ya serikali na chama.
Ushindi wake wa moja kwa moja katika eneo bunge la Lugari katika uchaguzi wa 1988 wa mlolongo, ulimfanya aamini zaidi nguvu za KANU.
Katika uchaguzi wa 1992, alishindwa na Apili Wawire wa FORD-Asili.
Kabla ya kuondoka Bungeni, Nabwera alihamishiwa Wizara ya Habari ambako aliendelea kutetea KANU.
Alifanya mabadiliko katika taasisi za habari akilenga kuhakikisha zinaunga mkono chama hicho kabla ya uchaguzi wa vyama vingi wa 1992.
Aliondoa Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Utangazaji la Kenya (KBC), zamani VoK, James Kangwana, pamoja na bodi yake kupitia ilani ya serikali na kuwaweka watu alioamini walikuwa waaminifu kwa KANU.
Nabwera pia alikosoa Benki ya Dunia kwa masharti yake makali ya misaada kwa Kenya, akipinga hasa pendekezo la kupunguza idadi ya wanafunzi waliojiunga na vyuo vikuu.