Habari

Ruto afufua maono ya hayati Raila katika Ruwaza yake ya 2060

Na JUSTUS OCHIENG August 16th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

RAIS William Ruto alipozindua mjadala wa kitaifa kuhusu mustakabali wa Kenya baada ya Ruwaza ya 2030 wiki hii, aliutaja kama juhudi mpya za kuwapa mwongozo wa muda mrefu utakaonufaisha vizazi vya sasa na vijavyo.

Hata hivyo, nyuma ya kauli za kuunda mwongozo mpya wa maendeleo, unafanana pakubwa na pendekezo la aliyekuwa Waziri Mkuu Raila Odinga kuhusu Kongamano la Kitaifa la Vizazi ambalo lilizinduliwa miezi michache kabla ya kifo chake.

Mipango yote miwili inaweka wananchi katikati ya maamuzi kuhusu mustakabali wa taifa.

Pia inakusudia kuwahusisha vijana, wataalamu, viongozi wa kaunti, wanavyuo, sekta ya biashara, mashirika ya kiraia na viongozi wa kidini katika kujadili mwelekeo wa Kenya.

Pendekezo la Raila lilijikita zaidi katika kutafuta suluhu kwa changamoto za kisiasa, kiuchumi na kiutawala zinazokabili taifa.

Kwa upande mwingine, mjadala wa Ruto unalenga kufafanua Kenya itakuwa taifa la aina gani baada ya kufikia mwisho wa mpango wa Ruwaza ya 2030.

Licha ya tofauti hizo, misingi ya miradi hiyo inaonekana kufanana kwa kiasi kikubwa.

Yote inatokana na imani kuwa mustakabali wa Kenya haupaswi kuamuliwa na wanasiasa wachache katika mikutano ya Nairobi pekee.

Ruto amependekeza mchakato wa kitaifa utakaowahusisha wadau kutoka sekta mbalimbali ili kuamua dira mpya ya taifa.

Kwa mujibu wa vyanzo vya Ikulu, Gavana wa Kisumu Profesa Anyang’ Nyong’o amepewa jukumu la kuongoza timu itakayobuni mfumo wa majadiliano hayo.

Timu hiyo itapendekeza namna mashauriano yatafanyika kutoka mashinani hadi kiwango cha kitaifa.

Muundo huo unafanana pakubwa na mpango ambao Raila alikuwa amependekeza mwaka 2025.

Akizungumza katika mahojiano akiwa nyumbani kwake Karen Julai 19, 2025, Raila alisema kongamano hilo lingeanzia katika vituo vya kupigia kura kabla ya kuendelea hadi ngazi za wadi, maeneo bunge na kaunti.

Hatimaye, wawakilishi wangekutana katika kongamano kubwa la kitaifa la takribani wajumbe 3,000 kutoka sehemu mbalimbali za nchi.
“Hilo lingekuwa baraza halisi la wananchi,” alisema Raila wakati huo.

Alisisitiza kuwa wananchi wa kawaida walipaswa kupewa nafasi ya kueleza changamoto zao na kuamua vipaumbele vya taifa kabla ya wanasiasa kuingilia mchakato huo.

Kwa upande wake, Ruto alipokuwa akizindua mjadala huo katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Kenyatta (KICC), alisisitiza mara kadhaa kwamba si mradi wa serikali bali wa wananchi.

“Huu si mradi wa serikali. Huu ni mradi wa wananchi,” alisema Rais.

Aliongeza kuwa serikali itatoa jukwaa na rasilimali lakini haitawalazimisha wananchi maamuzi ya kufanya.

Kauli hiyo inaendana kwa kiwango kikubwa na mawazo ambayo Raila alikuwa ametetea kuhusu umuhimu wa wananchi kutumia mamlaka yao ya kikatiba kuamua hatima ya taifa.

Raila alipendekeza kwamba nusu ya wajumbe katika mikutano ya mashinani wawe vijana hasa wa kizazi cha Gen Z. Naye Ruto amesema mjadala wa baada ya Ruwaza ya 2030 lazima uzingatie maslahi ya vijana ambao watarithi Kenya ya baadaye.

Hata hivyo, kuna tofauti muhimu.
Kongamano la Raila lilizaliwa wakati taifa lilikuwa linakabiliwa na malalamishi kuhusu utawala, ukosefu wa ajira, ufisadi na madai ya ukatili wa polisi. Hivyo lilikuwa na mwelekeo wa kisiasa na kikatiba zaidi.

Kwa upande mwingine, mjadala wa Ruto umejikita katika maendeleo ya muda mrefu na namna ya kuhakikisha Kenya inabaki na mwongozo mmoja hata baada ya mabadiliko ya serikali.

Naibu Rais Kithure Kindiki na Kiongozi wa Wengi katika Bunge la Kitaifa Kimani Ichung’wah wamependekeza kwamba mwongozo huo mpya upewe msingi wa kisheria ili serikali zijazo zisibadilishe mwelekeo wa taifa kila baada ya uchaguzi.

Hata hivyo, changamoto kubwa kwa utawala wa Ruto itakuwa kuwashawishi wakosoaji kwamba mchakato huo ni wa kweli na haujalenga kuendeleza ajenda za kisiasa za serikali iliyopo madarakani.

Baadhi ya viongozi wa upinzani tayari wanataka ukaguzi wa kina wa utekelezaji wa Ruwaza ya 2030 kabla ya kuanzishwa kwa mpango mwingine mpya.

Kifo cha Raila Odinga Oktoba 2025 kilikatiza ndoto ya kongamano lake la kitaifa kabla ya kutekelezwa. Sasa mjadala wa Ruto kuhusu Kenya baada ya Ruwaza ya 2030 unaonekana kufufua kwa namna fulani baadhi ya mawazo hayo, lakini kwa sura mpya ya maendeleo na mipango ya muda mrefu ya taifa.