Ruto kufungua rasmi kichinjio cha Sh1 bilioni kilichokamilika baada ya miaka 17
KICHINJIO cha kisasa mjini Isiolo cha thamani ya Sh1 bilioni kinatarajiwa kufunguliwa rasmi wiki ijayo, miaka 17 baada ya ujenzi wake kuanza.
Kichinjio hicho kilifanyiwa majaribio ya kufanya kazi mnamo Ijumaa.
Wakati wa majaribio hayo, ng’ombe, mbuzi na ngamia walichinjwa ili kupima ufaafu wa mashine na mifumo ya kisasa kabla ya uzinduzi wake unaotarajiwa kufanywa na Rais William Ruto.
Mradi huo ulianza mnamo 2009, huku serikali ya Kaunti ya Isiolo ikichangia Sh538 milioni na serikali kuu ikitoa Sh451 milioni.
Kichijio hicho kimejengwa kwenye ardhi ya ekari 500,000 na ina sehemu mbalimbali ambazo zitarahisisha na kuharakikisha shughuli za utayarishaji wa nyama.
Afisa Mkuu wa Idara ya Mifugo katika Kaunti ya Isiolo, Godana Dida, alisema ng’ombe 300, ngamia 100 na kondoo pamoja na mbuzi 2,500 wanaweza kuchinjwa kila siku kwa muda wa saa nane.
Msimamizi wa mradi huo, James Munyoki naye alisema kituo hicho kimejengwa kwa viwango vya kimataifa ili kuiwezesha Kenya kupanua mauzo ya nyama katika masoko ya nje.
“Kichinjio cha Isiolo ni miongoni mwa kile cha kisasa zaidi katika Kusini mwa Afrika. Tumefuata miongozo ya Shirika la Afya Duniani (WHO) na viwango vya kimataifa vya usalama na usafi wa nyama,” akasema Bw Munyoki.
Mtaalamu wa usimamizi wa majitaka, Dkt Lucy Murira, alisema kichinjio hicho kitakuwa kikisafishwa na kutumia tena zaidi ya lita milioni mbili za maji taka kila siku kupitia mfumo unaoondoa harufu mbaya.
Hata hivyo, Bw Dida alisema uwezo wa kuchinja mifugo 3,000 kwa siku unamaanisha kuwa Isiolo pekee haiwezi kukidhi mahitaji ya mifugo.
“Tunashirikiana na kaunti jirani kubaini maeneo ya usambazaji wa mifugo. Kwa ushirikiano wa kaunti za Kaskazini na maeneo jirani, tutatosheleza mahitaji ya kichinjio hicho,” akasema.
Kichinjio hicho kitategemea kaunti za wafugaji ambazo zina zaidi ya ng’ombe milioni tatu, kondoo na mbuzi milioni 12.9 na ngamia zaidi ya milioni tatu.
Mwenyekiti wa Chama cha Wafugaji wa Isiolo, Mohamed Wario, alisema mradi huo utawapa wafugaji soko la uhakika na kufungua nafasi za uwekezaji katika uzalishaji wa malisho na maeneo ya kunenepesha mifugo.