Habari

Raha tele walimu wakiongezwa mshahara mwezi huu

Na MERCY SIMIYU July 20th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WALIMU nchini wataanza kupokea nyongeza ya mishahara kuanzia malipo ya mwezi huu baada ya Tume ya Kuwaajiri Walimu (TSC) kutekeleza awamu ya pili ya Mkataba wa Makubaliano (CBA) wa miaka ya 2025–2029.
Marekebisho hayo ya mishahara, yaliyoanza kutumika Julai 1, 2026, yatawaongezea walimu pesa ya hadi Sh2,055 kwa mwezi kulingana na daraja lao la kazi.
Walimu wa madaraja ya C2 na C3 ndio watanufaika zaidi, huku Walimu wa Sekondari I katika daraja la C3 wakipata nyongeza ya juu zaidi.
Kupitia barua ya Julai 16, TSC iliagiza wakurugenzi wa elimu wa maeneo yote kuhakikisha viwango vipya vya mishahara vinaanza kutekelezwa mara moja hadi Juni 30, 2027.
Mkataba huo ni awamu ya pili ya makubaliano yaliyotiwa saini kati ya TSC na vyama vya walimu vya KNUT, KUPPET na KUSNET.
Walimu wataendelea kubaki katika madaraja yao ya sasa lakini watahamishiwa viwango vipya vya mishahara. Walimu ambao nyongeza yao ya kawaida ya kila mwaka huanza Julai 1 watapokea kwanza nyongeza hiyo kabla ya kuhamishiwa kwenye viwango vipya.
TSC ilisema walimu wote waliokuwa kazini kufikia Julai 1, 2026 watanufaika na mabadiliko hayo isipokuwa walimu wa mafunzo kwa vitendo (interns). Aidha, tarehe zao za nyongeza za kila mwaka zitaendelea kubaki kama zilivyokuwa.
Chini ya viwango vipya, Wakuu Wakuu wa Shule katika daraja la D5 sasa watapokea mshahara wa kati ya Sh133,351 na Sh164,977 kwa mwezi. Wakuu wa Shule waandamizi na Maafisa Wakuu wa Usaidizi wa Mtaala wa daraja la D4 watapata kati ya Sh120,016 na Sh148,480, huku Wakuu wa Shule na Naibu Wakuu wa daraja la D3 wakilipwa kati ya Sh107,634 na Sh131,405.
Walimu wa daraja la D2, wakiwemo Naibu Wakuu wa Shule II na Walimu Wakuu waandamizi, watapokea kati ya Sh93,883 na Sh114,322 kwa mwezi, huku walimu wa daraja la D1 pia wakinufaika na viwango hivyo vipya.
TSC ilieleza kuwa posho zote zinazolipwa kwa sasa zitaendelea bila mabadiliko. Hizo ni pamoja na posho ya nyumba, mazingira magumu, usafiri, mizigo, likizo ya kila mwaka na posho ya mwongozo kwa walimu wenye ulemavu pale inapohusika.
Naibu Katibu Mkuu wa KNUT, Hesbon Otieno, alipongeza hatua hiyo lakini akasema chama hicho kitapigania kipindi kifupi zaidi cha CBA ili walimu waweze kujadiliana kuhusu mishahara na maslahi yao mara kwa mara.
Aliongeza kuwa ingawa nyongeza hiyo italeta afueni kwa walimu, haitoshi kukabiliana kikamilifu na changamoto zinazowakabili, zikiwemo gharama ya juu ya maisha, uhaba wa walimu, kucheleweshwa kupandishwa vyeo na mzigo mkubwa wa kazi.
Otieno alisema KNUT tayari imewasilisha pendekezo la kufupishwa kwa muda wa utekelezaji wa CBA kwa Rais William Ruto na sasa mazungumzo yataendelea kati ya chama hicho, TSC na Wizara ya Elimu.
Kwa mujibu wa vyama vya walimu, pamoja na kuboreshwa kwa mishahara, serikali inapaswa kushughulikia pia changamoto nyingine zinazowakabili walimu kama vile uhaba wa wahudumu, huduma duni za matibabu, kuhudumu kwa muda mrefu katika nyadhifa za kaimu bila kunufaika na marupurupu yanayostahili pamoja na mazingira bora ya kazi ili sekta ya elimu iweze kuvutia na kuhifadhi walimu wenye taaluma na uzoefu.