Habari

Serikali yapunguza bei kwa ndururu mbili

Na NA JOHN MUTUA June 15th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WAKENYA inaonekana hawatapata nafuu ya juu zaidi kuhusu bei ya mafuta hivi karibuni baada ya serikali kutangaza kuwa imepunguza bei ya petroli kwa sumuni 0.22 pekee.
Suala la bei ya juu ya mafuta limekuwa likitumika kukashifu serikali wananchi wengi wakikasirikia bei za juu zinazoshuhudiwa nchini.
Mabadiliko hayo ya bei yanaonyesha kuwa serikali imetoa ruzuku ya juu zaidi kuliko miaka ya nyuma ili kuwakinga Wakenya na bei ambazo zingekuwa juu kuliko jinsi ilivyo kwa sasa.
Jana, serikali ilitangaza bei mpya ambapo dizeli nayo ilipungua kwa Sh10 kwa lita. Hii ina maana kuwa lita moja ya dizeli sasa itauzwa kwa Sh222.85 jijini Nairobi.
Baada ya kupungua kwa Sh0.22 petroli sasa itauzwa kwa Sh214.03 kwa lita. Bei ya mafuta taa itabaki bila mabadiliko ikiwa ni Sh146.93 kwa lita.
Serikali imetoa ruzuku ya Sh34.07 kwa kila lita ya dizeli ambazo hazijawahi kutolewa miaka ya nyuma, hatua ambayo imechangia kuzuia ongezeko zaidi la bei ya mafuta hayo.
Imechukua hatua hii wakati ambapo wananchi wameendelea kulalamikia gharama ya juu ya maisha inayochangiwa kwa kiasi kikubwa na bei ya juu ya mafuta.
Mwezi uliopita, Rais William Ruto alikuwa ameahidi kuwa bei ya dizeli ingepungua kwa Sh10. Hata hivyo, mabadiliko katika mfumo wa kuratibu bei za shehena za mafuta yanayoagizwa kutoka nje, ulizua hofu kuwa watumiaji wangenyimwa nafuu hiyo.
Kupungua kwa bei ya dizeli ni afueni kubwa kwa serikali katika juhudi zake za kudhibiti mfumko wa bei ambao umekuwa ukiongezeka. Mfumko huo sasa unakaribia kiwango cha juu cha asilimia 7.5 ambacho ni nafuu kwa serikali.
Mfumko wa bei, ambao ni kipimo cha gharama ya maisha, ulipanda hadi asilimia 6.7 mwezi uliopita, jambo lililoonyesha athari za bei ya juu ya dizeli iliyokuwa imefikia kiwango cha juu zaidi kuwahi kushuhudiwa.
“Katika kipindi kilichoangaziwa, bei za juu zilizoidhinishwa za petroli na dizeli zimepungua kwa Sh0.22 na Sh10 mtawalia, huku bei ya mafuta taa ikisalia bila mabadiliko,” akasema Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Kudhibiti Petroli (EPRA), Joseph Oketch jana asubuhi.
Gharama ya kuingiza dizeli nchini, ikijumuisha bei ya bidhaa na gharama za usafirishaji, iliongezeka kwa asilimia 0.21 hadi dola za Marekani 1,294.71 (Sh168,079.25) kwa kila mita ya ujazo mwezi uliopita kutoka dola 1,291.98 (Sh167,388.92) Aprili.
Kwa upande wa petroli, gharama ya kuingiza nchini ilipungua kwa asilimia 0.56 hadi dola 901.16 (Sh116,988.59) kwa kila mita ya ujazo kutoka dola 906.23 (Sh117,411.15) Aprili.
Kupungua kwa bei ya dizeli sasa kunageuza macho kwa watoa huduma za usafiri wa umma ili wapunguze nauli.
Hii ni kwa sababu nauli ilipanda mwezi uliopita baada ya bei ya mafuta hayo kufikia kiwango cha juu zaidi katika tathmini ya kila mwezi inayomalizika leo.
Mwezi uliopita, wahudumu katika sekta ya uchukuzi wa umma waliandaa mgomo wa siku mbili wakipinga bei ya juu ya dizeli, hatua iliyolazimu serikali kufanya kupunguza bei kwa Sh10.
Baadaye, Rais Ruto aliahidi kupunguzwa kwa ziada kwa Sh10 katika bei zilizotangazwa leo, huku serikali yake ikijitahidi kudhibiti malalamishi yanayoongezeka kutoka kwa wananchi kuhusu gharama kubwa ya maisha.