Habari

Likizo ya Gachagua kumwacha mgombea wa DCP Ol Kalou kwenye mataa

Na MOSES NYAMORI June 15th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

ALIYEKUWA Naibu wa Rais Rigathi Gachagua kuanzia leo atajiondoa kwa muda katika shughuli za kisiasa na kujifungia katika makazi yake ya Wamunyoro, Kaunti ya Nyeri, kwa siku 45.
Hatua hiyo itamweka mbali na mikutano ya kisiasa, ikiwemo kampeni ya uchaguzi mdogo wa eneo la Ol Kalou.
Uchaguzi huo mdogo, ambao umechukuliwa kama mchuano wa kisiasa kati ya DCP na UDA katika eneo la Mlima Kenya kabla ya 2027, umepangwa kufanyika Julai 16, 2026, siku 31 kutoka sasa.
“Hamtaniona popote katika mikutano ya kisiasa kwa siku 45 zijazo,” alisema Bw Gachagua Jumatano wiki jana.
Alisema baada ya kukamilisha ziara yake ya siku tatu eneo la Magharibi mwa Kenya jana, hatashiriki katika shughuli za kisiasa.
Hii itampa muda wa kukutana na viongozi na kupokea maoni jinsi Muungano wa Upinzani unaweza kuafikiana kuhusu mgombea mmoja wa urais atakayemenyana na Rais Ruto.
Wadadisi wa siasa wanaona kuwa uamuzi wa Bw Gachagua kujitenga kwa muda na shughuli za kisiasa, ikiwemo kampeni za uchaguzi mdogo, unaweza kumdhuru mgombea wa DCP, Bw Kamau Ngotho.
Wanasema uwepo wake katika kampeni ungechochea hisia za kumpinga Rais Ruto na kuweka msingi wa siasa za uchaguzi mkuu wa 2027.
Wengine wanaamini kuwa hatua hiyo ni mikakati ya kisiasa ya kujiepusha na lawama za moja kwa moja iwapo mgombea wa DCP atashindwa.
UDA imenogesha kampeni zake katika eneo hilo ambalo limekuwa likichukuliwa kama ngome ya DCP.
Matokeo ya uchaguzi huo mdogo yanaonekana kuwa muhimu kwa Bw Gachagua na DCP kwa kuwa yatia umaarufu wake kwenye mizani. Jumla ya wagombea tisa kutoka vyama mbalimbali walipitishwa na Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) kushiriki katika uchaguzi huo. Uchaguzi mdogo wa Ol Kalou unatoa nafasi ya pili kwa makabiliano ya moja kwa moja kati ya DCP ya Bw Gachagua na UDA ya Rais Ruto katika uchaguzi mdogo.
Mwezi uliopita, DCP ilishindwa na UDA katika uchaguzi mdogo wa ubunge wa Emurua Dikirr.
UDA pia ilishinda katika chaguzi ndogo za Mbeere North ambapo Muungano wa Upinzani uliunga mkono mgombea wa Democratic Party (DP).
Washirika wa Bw Gachagua waliiambia Taifa Leo kwamba DCP ina imani kubwa ya kushinda kiti hicho licha ya mpango wake wa kujitenga kwa siku 45. Walisema Seneta wa Nyandarua John Methu ataongoza kampeni hizo, lakini iwapo kutakuwa na haja, hawatasita kumwomba Bw Gachagua kujiunga na kampeni.
Mbunge wa Embakasi Central Benjamin Gathiru almaarufu Mejja Donk alisema hakuna kinachomzuia Bw Gachagua kushiriki kampeni na kuzungumza na wapigakura wa Ol Kalou kabla ya uchaguzi.
“Iwapo kutakuwa na haja, tutamwita kuongeza nguvu. Lakini kwa sasa tuna imani ya kushinda. Watu wa eneo hilo tayari wameamua ni mgombea gani wanayetaka awaongoze,” alisema.
Maoni kama hayo yalitolewa na Mbunge wa Gatanga Edward Muriu ambaye alieleza kuwa kipindi hicho cha siku 45 ni cha kupokea maoni na hakimzuii kabisa Bw Gachagua kushiriki kampeni iwapo kutakuwa na ulazima.