SHA yazima hospitali ya MP Shah kwa siku 90 kufuatia malalamishi ya wateja
MAMLAKA ya Afya ya Kijamii (SHA) imezima Hospitali ya MP Shah katika mpango wa bima ya afya wa serikali kwa muda wa siku 90 baada ya kupokea malalamishi mengi kutoka kwa wagonjwa waliodai kutozwa fedha kwa huduma ambazo zinapaswa kugharamiwa kikamilifu na hazina ya bima ya afya.
Katika barua aliyoandikia hospitali hiyo Juni 23, 2026 na kutiwa saini na Afisa Mkuu Mtendaji wa SHA, Dkt Mercy Mwangangi, mamlaka hiyo ilisema imepokea malalamishi mengi kutoka kwa wananchi kuhusu jinsi huduma za afya zinavyotolewa katika hospitali hiyo.
Kwa mujibu wa SHA, baadhi ya wagonjwa walilazimika kulipa pesa kutoka mifukoni mwao kwa huduma ambazo tayari zimejumuishwa katika mpango wa SHIF.
“Malalamishi yanaonyesha kuwa, baadhi ya wanaonufaika walitozwa ada kwa huduma ambazo zinapaswa kulipiwa kikamilifu chini ya mpango wa SHIF. Pia kumekuwa na visa vya hospitali kudai kiwango kidogo kuliko kinachostahili kutoka kwa SHA, hali inayowaachia wagonjwa mzigo wa gharama,” ilisema sehemu ya taarifa hiyo.
Miongoni mwa visa vinavyochunguzwa ni cha mtoto anayejulikana kama Baby Thompson ambaye alidaiwa kutozwa Sh83,308 mnamo Mei 3, 2026 kwa huduma ambazo zilipaswa kulipiwa na SHIF.
Katika kisa kingine, mgonjwa aliyefahamika kama Guyo Rendille alidaiwa kulazimika kulipa gharama za matibabu licha ya kuwa mwanachama wa SHIF aliyekuwa amelipa michango yote inayohitajika.
Pia, kuna visa viwili vinavyohusisha wagonjwa waliotambuliwa kama P.N. Gupta na Vyonne Gakii ambapo SHA inachunguza madai ya hospitali kudai kiwango cha chini kuliko gharama halisi za huduma, jambo ambalo lilisababisha wagonjwa kubeba sehemu ya mzigo wa kifedha.
Kutokana na malalamishi hayo, SHA imezuia hospitali hiyo kupokea, kutibu au kulaza wagonjwa wanaotegemea bima ya SHIF hadi uchunguzi utakapokamilika.