Hatuna haja na maandamano Nairobi, mbunge wa ODM asema
MWENYEKITI wa ODM Kaunti ya Nairobi na Mbunge wa Makadara, George Aladwa, Jumatano alitangaza kuwa wafuasi wa chama hicho hawatashiriki katika maandamano ya Gen Z mnamo Alhamisi.
Mbunge huyo alisisitiza kuwa ODM inaunga mkono utawala wa Rais William Ruto kufuatia makubaliano yaliyozaa Serikali Jumuishi na hawana haja na maandamano.
“Kama viongozi wa ODM Nairobi, tunapinga vikali maandamano haya kwa sababu hayatoi suluhu kwa changamoto zinazowakabili Wakenya. Wananchi wa Nairobi wanahitaji amani, ajira, fursa za kufanya biashara na maendeleo, si vurugu, hofu na uharibifu,” akasema Bw Aladwa.
Akizungumza jijini Nairobi Jumatano, Bw Aladwa alisema chama hicho kimeamua kutoshiriki maandamano ya Gen Z kwa kuwa serikali iliyopo madarakani inaendelea kutekeleza ahadi zake kwa wananchi.
“Tuna kumbukumbu chungu za yaliyotokea wakati wa maandamano yaliyopita ambapo mali ya mamilioni ilipotea. Maisha yalipotea na familia nyingi ziliachwa zikiomboleza huku biashara nazo zikiporwa,” akasema Bw Aladwa
Mbunge huyo anayehudumu muhula wa pili alisema wawekezaji walijiondoa nchini na wengi wakasalia nyumbani kutokana na utovu wa usalama, hali ambayo haifai kujirudia.
“ODM imefanya uamuzi wa kimakusudi wa kutumia mazungumzo na ushirikishaji wa umma kutatua masuala yanayowakabili Wakenya,” akaongeza.
Bw Aladwa alisema maandamano yaliyopita yaliwaathiri zaidi wananchi wa kawaida, wafanyabiashara wadogo, mama mboga, wahudumu wa bodaboda na vijana wanaojitahidi kujipatia riziki halali.
“Tunaunga mkono serikali kwa sababu imeonyesha nia ya kuharakisha utekelezaji wa miradi ya maendeleo, kufufua uchumi na kuhakikisha Wakenya wananufaikia utawala huu,” akasema.
Aligusia suala la fidia ya Sh2 bilioni ambazo zimetengwa kwenye bajeti kwa wahanga wa maandamano yaliyopita, akisema hiyo inaonyesha serikali inawajali walioumia wakipigania haki.
Kwa hivyo, alisema makabiliano zaidi yatavuruga amani nchini huku akisema masuala yanayoibuliwa kuhusu uongozi wa nchi yatatatuliwa tu kupitia mashauriano.